• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 6:55 PM
Rais wa Haiti auawa kwa kupigwa risasi nyumbani kwake

Rais wa Haiti auawa kwa kupigwa risasi nyumbani kwake

Na AFP

PORT-AU-PRINCE, Haiti

WATU wasiojulikana Jumatano waliingia katika makazi ya Rais Jovenel Moise wa Haiti na kumpiga risasi, ilisema serikali ya taifa hilo.

Kaimu Waziri Mkuu, Claude Joseph, alisema watu hao waliingia kwenye makazi hayo mwendo wa saa saba usiku na kumuua kwa kumfyatulia risasi.

“Watu wasiojulikana waliingia katika makazi ya kibinafsi ya Rais na kumpiga risasi. Vile vile walimjeruhi mkewe, ambaye ashakimbizwa hospitalini kupokea matibabu,” ikasema taarifa iliyotolewa na afisi yake.

Kiongozi huyo alisema ndiye anayeiongoza nchi hiyo kwa sasa. Alikashifu vikali kitendo hicho huku akiwaomba raia kudumisha utulivu.

Alisema polisi na vikosi vya usalama nchini humo vimeanza uchunguzi kubaini chanzo cha kitendo hicho.

Marehemu amekuwa akiliongoza taifa hilo kwa nguvu baada ya chaguzi za bunge kucheleweshwa katika hali tatanishi. Chaguzi hizo zilikuwa zimepangiwa kufanyika mnamo 2018.

Ni hali iliyozua mzozo na utata mkubwa ambao umekuwepo hadi sasa. Haiti ndilo taifa maskini zaidi katika eneo la Carribean.

You can share this post!

CHAKISE; Nuru inayovumisha mawimbi ya Kiswahili Shuleni...

Huenda Guardiola akose kizibo cha Aguero