• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 10:10 AM
Bawabu aliyeingia kwa nyumba aliyolinda kusaka chakula motoni

Bawabu aliyeingia kwa nyumba aliyolinda kusaka chakula motoni

Na RICHARD MUNGUTI

BAWABU aliyeingia ndani ya nyumba aliyokuwa analinda kusaka chakula anasubiri uamuzi ikiwa atasukumwa gerezani au la.

Boniface Ngare alishtakiwa mbele ya hakimu mkazi Sharon Maroro alikiri aliingia ndani ya nyumba ya Bw Daniel Kamau kwa lengo la kuiba.

Mshtakiwa alikuwa ameajiriwa kulinda jumba la Bw Kamau katika mtaa wa Lang’ata.

Mnamo Julai 1, 2021 mshtakiwa alikutwa ndani ya nyumba na mjakazi akisaka chakula.

Mjakazi huyo alimwita Bw Kamau na kumweleza kulikuwa na mtu ndani ya nyumba ambaye nia yake ilikuwa haijulikani.

Mwajiri wa Bw Ngare alifahamishwa na alipokamatwa mlinzi huyo aliungama kwamba “ alikuwa anahisi njaa na ndipo aliamua kuingia mle chumbani mwa mlalamishi kusaka chakula.”

Mahakama ilielezwa mshtakiwa alikiri alikuwa anahisi njaa na ndipo akaamua kuingia mle ndani kutafuta chakula.

“Nilihisi njaa mithili ya kuangamia ndipo nikaamua na liwe liwalo nikaingia mle nyumbani nitafute chakula. Nilikutwa ndani ya chumba ambapo mlalamishi anahifadhi pombe kali,” hakimu alifahamishwa.

Mshtakiwa akijitetea alimweleza hakimu, “Mimi nilihisi njaa nusura nife ndipo nikaamua kuingia ndani ya nyumba kutafuta chakula.”

Mshtakiwa aliomba msamaha na kuomba korti “ipitishe hukumu afungwe nje aendelee kusaidia familia yake.”

Bi Maroro aliamuru idara ya urekebishaji tabia imhoji mshtakiwa pamoja na watu wa familia ndipo ukweli ukithiri.

Hakimu atatoa uamuzi mnamo Julai 14, 2021.

You can share this post!

Wezi wa nyaya za stima bungeni taabani

Je, mkataba wa kibiashara baina ya Kenya na Uingereza...