• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
JAMVI:  Kalonzo alivyowazidimaarifa magavana wa Ukambani

JAMVI: Kalonzo alivyowazidimaarifa magavana wa Ukambani

Na BENSON MATHEKA

Juhudi za magavana wa kaunti tatu za Ukambani kuzima kiongozi wa chama cha Wiper Kalonzo Musyoka asiwike kwenye ziara ya Rais Uhuru Kenyatta eneo lao ziligonga mwamba makamu rais huyo wa zamani alipomshawishi kiongozi wa nchi kubadilisha nia yake ya kufuta ziara hiyo.

Ikulu ilitangaza Jumatatu wiki hii kwamba Rais alikuwa ameahirisha ziara hiyo kwa sababu ya hofu ya kukiuka kanuni za kuzuia corona lakini ikasemekana ni tofauti za magavana hao na Bw Musyoka zilizofanya rais kuchukua hatua hiyo.

Magavana Alfred Mutua wa Machakos, Charity Ngilu wa Kitui na Kivutha Kibwana walikuwa wamedai kwamba Bw Musyoka alitaka kutumia miradi ambayo Rais alitembelea kupigia debe azima yake ya urais kwenye uchaguzi mkuu wa 2022 na wakaonya kuwa hawangemruhusu kufanya hivyo.

“Hatutarajii wanasiasa wasio na la kufanya kutumia ziara hiyo kuonekana wakitembea pamoja na rais,” Dkt Mutua alisema.

Inasemekana viongozi walitofautiana kuhusu miradi ambayo ilipaswa kufunguliwa na Rais, hatua ambayo ilichangia ikulu kuahirisha ziara hiyo japo ilisema ni kwa sababu ya hofu ya corona.

Duru zinasema kwamba magavana hao hawakutaka Rais Kenyatta kumuidhinisha Bw Musyoka kama msemaji wa jamii ya Wakamba.

Wamekuwa wakimlaumu Bw Musyoka kwa kutumia madiwani wa chama chake walio wengi katika mabunge ya kaunti zao kuhujumu ajenda za serikali zao.

Imeibuka kuwa baada ya Ikulu kutangaza kuwa ziara ya Rais katika kaunti za Ukambani ilikuwa imeahirishwa, Bw Musyoka alimpigia simu Rais Kenyatta na kumshawishi abadilishe nia.

Kulingana na mwandani mmoja wa kiongozi huyo wa Wiper, Rais Kenyatta alikubali na ndipo akaita mkutano wa viongozi wa Ukambani Jumanne jioni ambapo alikubali kuzuru eneo hilo kwa kuzingatia kanuni za kuzuia msambao wa corona.

“Bw Musyoka alihisi kwamba kuahirishwa kwa ziara ya Rais eneo la Ukambani mara ya tatu kungetoa taswira mbaya kwa uongozi wa eneo hilo na hasa kwake kama msemaji wa jamii na ndio sababu aliwasiliana na rais. Anafahamu kwamba magavana hao wana azima zao na wanafikiri anatumia miradi waliyoanzishwa kujipigia debe lakini sivyo,” asema mwandani huyo aliyeomba tusitaje jina lake.

Kwenye mkutano wa Jumanne jioni, Rais Kenyatta alikubali kuzuru miradi ya serikali ya kitaifa katika eneo hilo Ijumaa lakini kwa kuzingatia kanuni za corona.

Hii, kulingana na wadadisi wa siasa, ilihakikisha kwamba hatahutubia mikutano ya kisiasa jambo ambalo ni pigo kwa magavana waliotaka kumpiga kumbo Bw Musyoka.

“Kwa kufanya hivi, rais aliepuka hali ambapo viongozi wa eneo hilo wangeendeleza siasa zao za mgawanyiko mbele yake,” alisema.

Ingawa awali ziara hiyo ilipangiwa kuchukua siku mbili, ilipunguzwa kuwa ya siku moja. Rais Kenyatta alizuru jiji la kitekinolojia la Konza na bwawa la Thwake katika kaunti za Machakos na Makueni.

Ingawa ziara hiyo ilishirikisha viongozi wa kaunti hizo, Bw Musyoka alitekeleza wajibu muhimu hatua ambayo wadadisi wa siasa wanasema ilikuwa ujumbe kwamba rais anamtambua kama kigogo wa siasa eneo hilo.

“Kwa maoni yangu, magavana hao hawakuweza kuzima Bw Musyoka walivyonuia hasa Gavana Mutua na Gavana Kibwana ambao wananuia kugombea urais. Angalau Gavana Ngilu amekuwa akihimiza Musyoka kuungana na vinara wenzake wa NASA katika siasa za kitaifa,” asema mdadisi wa siasa za Ukambani Bw Nicholas Kitetu.

Mnamo Jumatano, Bw Musyoka aliungana na baadhi ya viongozi wanaomuunga mkono kuzuru miradi ya serikali ya kitaifa ambayo Rais alitembelea Ijumaa na kupuuza madai kwamba anaitumia kujipigia debe.

“Wanachoogopa ( wapinzani) ni umaarufu wa Wiper na azima yangu ya urais. Wanajua haturudi nyuma,” alisema Bw Musyoka na kuongeza kuwa ziara yake ilikuwa ya kukagua miradi hiyo kabla ya rais kuitembelea.

Kulingana na Bw Kitetu, japo Rais aliepuka kuvunja kanuni za kuzuia corona kwa kutohutubia mikutano ya kisiasa, magavana wanaompiga vita Bw Musyoka wamepata pigo.

“Hakuna kati yao anaweza kudhihirishia rais kwamba ameshinda Bw Musyoka kwa umaarufu. Hilo ni bayana. Ikiwa ni kweli Bw Musyoka alimpigia simu rais kumshawishi abadilishe nia na kuzuru eneo hilo bila kuhutubia mikutano ya kisiasa, aliwashinda magavana hao waliodhani angetumia mikutano hiyo kujipigia debe kwa umma,” asema.

You can share this post!

JAMVI: Uhuru, Ruto mbioni kudhihirisha ubabe Mlima Kenya

UDA kufanya uchaguzi wa mashinani Oktoba – Muthama