• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 3:03 PM
Kipa Gianluigi Donnarumma wa Italia atawazwa Mchezaji Bora wa Uefa Euro 2020

Kipa Gianluigi Donnarumma wa Italia atawazwa Mchezaji Bora wa Uefa Euro 2020

Na MASHIRIKA

KIPA Gianluigi Donnarumma wa Italia alitawazwa Mchezaji Bora wa kipute cha Euro 2020, mashindano yaliyokamilika rasmi Julai 11, 2021.

Mlinda-lango lango huyo mwenye umri wa miaka 22 anatarajiwa kuingia katika sajili rasmi ya Paris Saint-Germain (PSG) muhula huu baada ya mkataba wake na AC Milan ya Ligi Kuu ya Italia (Serie A) kutamatika rasmi mwishoni mwa msimu wa 2020-21.

Donnarumma alipangua mikwaju miwili ya penalti katika fainali ya Euro iliyoshuhudia Italia ikizamisha chombo cha Uingereza baada ya kuambulia sare ya 1-1 mwishoni mwa muda wa kawaida na wa ziada.

Mlinda-lango wa Italia Gianluigi Donnarumma (kati-kushoto) amkumbatia mlinda-lango wa Italia Salvatore Sirigu (kati-kulia) mara baada ya ushindi kwenye fainali kali ya Uefa Euro 2020 iliyokutanisha Italia na Uingereza uwanjani Wembley jijini London, Julai 11, 2021. Picha/ AFP

Ufanisi huo wa Italia uliwavunia taji la kwanza la Euro tangu 1968.

Donnarumma ambaye hakufungwa katika mechi tatu za kampeni za Euro mwaka huu, aliwazidi ujanja Jadon Sancho na Bukayo Saka walioaminiwa fursa za kuchanja penalti za mwisho za Uingereza.

Ndiye kipa wa pili katika historia kuwahi kujizolea tuzo hiyo kwenye Euro baada ya aliyekuwa ‘nyani’ wa Denmark, Peter Schmeichel mnamo 1992.

Donnarumma aliwajibishwa na Italia kwa kipindi cha dakika 719 kwenye fainali za Euro mwaka huu na akawa mchezaji wa pekee aliyechezeshwa na kocha Roberto Mancini katika kila mojawapo ya mechi kwenye kipute hicho.

“Tulijituma vilivyo bila ya kukata tama. Tulianza vyema kampeni hizi kwa kuweka wazi malengo yetu. Ingawa hatukutarajia ufanisi huu, hili ni taji ambalo nahisi kwamba tulistahili kulitwaa,” akasema Donnarumma.

Gonzalez ‘Pedri’ Lopez wa Uhispania alitawazwa Chipukizi Bora wa kipute cha Euro 2020, mashindano yaliyocheleweshwa kwa sababu ya janga la Covid-19.

Pedri mwenye umri wa miaka 18 alikosa kuwajibikia Uhispania kwa dakika moja pekee kwenye Euro baada ya kuondolewa uwanjani katika sekunde za mwisho za muda wa ziada wakati wa robo-fainali dhidi ya Uswisi. Kabla ya kuwakilisha Uhispania kwenye Euro mwaka huu, alikuwa amevalia jezi za kikosi hicho mara nne pekee katika mapambano ya timu ya watu wazima.

“Hakuna mwanasoka yeyote katika historia ya Euro ambaye amefanya kitu ambacho Pedri amekifanya kwenye kipute hicho mwaka huu. Ana umri wa miaka 18 pekee na dalili zote zinaashiria kwamba anafuata nyayo za nguli Andres Iniesta. Ana kipaji adhimu na anaridhisha sana,” akasema kocha wa Uhispania, Luis Enrique.

Cristiano Ronaldo wa Ureno alitawazwa Mfungaji Bora wa Euro mwaka huu. Ingawa idadi ya mabao aliyofunga yaliwiana na yale yaliyopachikwa wavuni na Patrik Schick wa Jamhuri ya Czech, Ronaldo aliibuka kileleni kwa sababu alichangia goli jingine katika mechi ya Kundi F dhidi ya Ujerumani.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO 

You can share this post!

Modern Coast, Mombasa Raha zasitisha huduma

Italia wakomoa Uingereza na kutwaa ubingwa wa Uefa Euro 2020