• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 12:58 PM
Mgombea wa ubunge Kiambaa kwa tiketi ya UDA alia serikali kumhangaisha

Mgombea wa ubunge Kiambaa kwa tiketi ya UDA alia serikali kumhangaisha

Na SAMMY WAWERU

MWANIAJI wa kiti cha ubunge Kiambaa anayepeperusha bendera ya United Democratic Alliance (UDA) John Njuguna Wanjiku ameishtumu serikali kwa kile anadai ni kulemaza jitihada zake kusaka kura.

Bw Njuguna amesema mikutano yake ya hadhara inadhalilishwa na serikali, huku mgombea wa Jubilee, Kariri Njama akiruhusiwa kuendesha kampeni bila vikwazo.

“Jumapili tulipangia kudaandaa mechi ya soka ya ‘mahastla’, ila tulizuiwa kuingia uwanjani,” Njuguna akalalamika.

Kulingana na mgombea huyu, UDA, chama kinachohusishwa na Naibu wa Rais, Dkt William Ruto, mchuano kati ya Karuri United na Simba FC ulipaswa kugaragazwa katika uga wa Shule ya Msingi ya Karuri, iliyoko Kiambaa, Kaunti ya Kiambu.

“Tulikatazwa kuleta wafuasi wetu pamoja. Maafisa wa polisi walimwagwa tukazuiwa kuingia,” akasema, akieleza kushangazwa kwake na Jubilee kuandaa mechi bila vikwazo.

“Tuliona Jubilee iliandaa mechi yake chini ya ulinzi. Serikali inatumia raslimali zake kufanyia kampeni mwaniaji wa Jubilee, ni kinyume cha sheria za uchaguzi,” akasema.

Bw Njuguna aidha amelalamikia hatua ya serikali kutumia wazee wa kijiji na machifu kung’oa vibango vyake vya kampeni.

Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imeratibu uchaguzi mdogo wa Kiambaa kufanyika mnamo Alhamisi, Julai 15.

Kiti hicho kilisalia wazi Machi 2021 kufuatia kifo cha aliyekuwa mbunge, Bw Paul Koinange.

You can share this post!

Cristiano Ronaldo aibuka Mfungaji Bora wa Uefa Euro 2020

Mashabiki wapokea kikosi cha Italia kwa shangwe na mbwembwe...