• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 AM
Wanawake watwaa majukumu ya kiume wazee wakilewa tu!

Wanawake watwaa majukumu ya kiume wazee wakilewa tu!

WANDERI KAMAU na STEVE NJUGUNA

ATHARI za matumizi ya mihadarati miongoni mwa vijana katika eneo la Mlima Kenya zimeanza kupita mipaka kiasi kwamba, wanawake sasa wamechukua majukumu yanayotekelezwa na wanaume.

Ingawa kuna majukumu yanayopaswa kutekelezwa na wanaume kulingana na mtindo wa kimaisha wa jamii za Kiafrika, hali imebadilika katika eneo hilo.

Wanawake wanasema “wamegeuka kuwa wanaume” kwani waume wao wamezamia kwenye ulevi na matumizi ya dawa za kulevya.

Ni hali ambayo imezua mdahalo na wasiwasi mkubwa, baada ya picha za wanawake wakichimba kaburi kusambaa katika mitandao ya kijamii.

Kisa hicho kilifanyika katika eneo la Wiyumiririe, Kaunti Ndogo ya Ngorika, Kaunti ya Nyandarua.

Kulingana na wenyeji, wanawake waliamua kuchukua jukumu hilo baada ya vijana waliotarajiwa kushiriki kwenye kazi hiyo kukataa kufika wakidai “kutukanwa na chifu wa eneo hilo.”

“Walikataa kushiriki wakisema chifu aliwakosea heshima kwa kuwaita wazembe na walevi kutokana na uraibu wao wa kuzamia kwa mihadarati,” akasema Bi Mary Wanjira ambaye ni mkazi, kwenye mahojiano na ‘Taifa Leo.’

Ingawa vijana walidai “kukosewa heshima”, kisa hicho kimeibua hofu kuhusu kukithiri kwa ulevi miongoni mwa wanaume katika ukanda huo.

Hilo pia linajiri baada ya mwanamume mmoja kufariki Jumapili mjini Nyahururu huku wengine tisa wakilazwa hospitalini baada ya kunywa pombe yenye sumu.

Eneo la Mlima Kenya linazishirikisha kaunti kumi, ambazo ni Nyeri, Nyandarua, Meru, Tharaka-Nithi, Embu, Laikipia, Murang’a, Kiambu, Kirinyaga na Nakuru.

Hata hivyo, athari za ulevi zimekuwa zikionekana sana kuathiri eneo la Kati.

Kulingana na aliyekuwa Mshirikishi Mkuu wa Mfumo wa Nyumba Kumi, Bw Joseph Kaguthi, inasikitisha kuwa vijana wengi wanaendelea kujiingiza kwenye ulevi licha ya juhudi ambazo zimekuwa zikiendeshwa na serikali kubuni ajira.

Anasema kwa muda mrefu, vijana wamekuwa wakitoa kisingizio cha ukosefu wa ajira na ugumu wa maisha kama sababu kuu ya kujiingiza kwenye uraibu huo.

“Serikali imejizatiti kuimarisha vita dhidi ya maovu hayo kupitia ujenzi wa vyuo vya kiufundi kuwawezesha vijana kujiendeleza kitaaluma. Kinyume na ilivyokuwa awali, hawahitajiki kulipa ada kubwa,” akasema.

Bw Kaguthi anawalaumu wazazi na walezi wa vijana, akisema hawatekelezi majukumu yao ya ulezi ifaavyo.

Anapendekeza wadau wote katika jamii kuungana ili kuhakikisha ushindi dhidi ya janga hilo.

Wakazi mbalimbali kutoka ukanda huo waliozungumza na ‘Taifa Leo’ waliwalaumu baadhi ya maafisa wa utawala, hasa machifu, kwa kuruhusu utengenezaji pombe kuendelea bila kukabiliwa hata kidogo.

Katika Kaunti ya Nyandarua, wenyeji walisema polisi huwa wanashirikiana na machifu kuchukua hongo kutoka kwa watengenezaji pombe hizo.

“Inasikitisha hata idadi ya watoto wanaoenda shuleni imepungua sana kwani vijana wengi wanachelewa kuoa kutokana na matumizi ya mihadarati. Idadi ndogo ya watoto katika shule zetu ni kama robo pekee ikilinganishwa na ilivyokuwa katika miaka ya awali,” asema Mzee Gitonga Mwangi, ambaye ni mwanachama wa Mfumo wa Nyumba Kumi katika eneo la Kinangop.

Mnamo 2015, Rais Uhuru Kenyatta alianza kampeni kali kukabili ulevi katika ukanda huo, akiutaja kuwa kizingiti cha maendeleo.

You can share this post!

Kiunjuri ajipendekeza kuwa naibu wake Ruto

Nairobi, kaunti za Mlima Kenya zaorodheshwa tajiri zaidi...