• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 3:03 PM
Je, IEBC yafaa kuanza kujiandaa kwa kura ya maamuzi kabla ya uamuzi wa mahakama kuhusu rufaa ya BBI?

Je, IEBC yafaa kuanza kujiandaa kwa kura ya maamuzi kabla ya uamuzi wa mahakama kuhusu rufaa ya BBI?

Na CHARLES WASONGA

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) inaonekana kuanza maandalizi ya kura ya maamuzi ilhali hatima ya mchakato huo haijaamuliwa na mahakama ya rufaa.

Hii ni baada ya tume hiyo, Jumatano, kutangaza zabuni ya ununuzi karatasi za kupigia kura zitakazotumika katika kura ya maamuzi na uchaguzi mkuu ujao.

Kulingana na tangazo lilichapishwa katika gazeti la ‘Daily Nation‘ IEBC inazitaka kampuni zenye uwezo wa kufanya kazi hiyo ziwasilishe maombi kwa idara ya ununuzi kupitia barua pepe.

“IEBC inaalika zabuni za uwasilishaji wa karatasi za uchaguzi, sajili za wapiga kura, fomu za kutangaza matokeo katika vituo vya kupigia kura, fomu za kutangaza matokeo ya uchaguzi na kura ya maamuzi katika vituo vya kuanzia ngazi ya eneo bunge, wadi hadi kitaifa,” likasema tangazo hilo likiongeza kuwa zabuni hiyo itadumu kwa miaka mitatu.

Tangazo hili la IEBC linaonyesha kuwa IEBC inajiandaa kwa kura ya maamuzi kuhusu mswada wa marekebisho ya katiba ya BBI hata ingawa Mahakama ya Rufaa haijatoa uamuzi wake kuhusu iliyowasilishwa kupinga uamuzi mahakama kuu iliyoharamisha mchakato huo.

Majaji wa mahakama kuu, Joel Ngugi, George Odunga, Jairus Ngaah, Chacha Mwita na Teresia Matheka katika uamuzi waliotoa Mei 13, pia walisema kuwa mchakato wa BBI ulikiuka Katiba ya Kenya.

Japo ni taratibu ya kawaida kwa IEBC kutangaza zabuni ya uchapishaji na uwasilishaji wa karatasi za kura na bidhaa nyinginezo hitaji uchaguzi mkuu unapokaribia, uagizaji wa bidhaa za kuendesha kura ya maamuzi ni dalili kwamba tume hiyo pia inajiandaa kwa zoezi hilo tata.

Uamuzi kuhusu kesi hiyo ya rufaa iliyowasilisha na Rais Uhuru Kenyatta pamoja na kiongozi wa ODM Raila Odinga, utatolewa mnamo Agosti 20, 2021.

Tangazo hilo la IEBC limekasirisha wakosoaji wa mchakato wa marekebisho ya Katiba wakisema imetolewa kwa nia mbaya na inakiuka amri ya mahakama kuu “ambayo haitajabatilishwa”.

“Tunaona nia mbaya katika tangazo hili. Aidha ya bidhaa ambazo IEBC inataka kununua zinaonyesha kuwa tume hii imekiuka amri ya mahakama kuu ambayo iliizuia kuandaa kura ya maamuzi,” akasema mawakili Ian Mwiti na Dudley Ochiel waliowakilisha Jack Mwimali aliyepinga kesi iliyowasilishwa na Rais Kenyatta na Bw Odinga katika mahakama ya rufaa.

“Pia kuna agizo la mahakama linalozuia tume kuanza maandalizi yoyote ya kura ya maamuzi. Lakini IEBC imepuuza agizo hili. Imetangaza zabuni ya ununuzi wa bidhaa kuendesha kura ya maamuzi. Hatua hii imechukuliwa kwa nia mbaya,” akasema Bw Mwiti.

Alisema IEBC ilifaulu tu kuzuia utekelezaji wa uamuzi kwamba haiwezi kuendeleza shughuli zake kwa sababu haina idadi tosha ya makamishna.

Na Bw Ochiel alisema kuwa mahakama kuu ilizuia IEBC kufanya chochote kuhusiana na suala la uhalali wa kura ya maamuzi ambalo bado halijaamuliwa na mahakama ya rufaa.

Wakili huyo pia alisema hatua ya IEBC kutangaza zabuni ya ununuzi wa bidhaa za uchaguzi inaonyesha kuwa tume hiyo imeonyesha kuwa inafahamu uamuzi wa mahakama ya rufaa.

“Hatua hii ya IEBC pia inaandaa mazingira bora kwa watetezi wa mchakato wa marekebisho ya katiba, jambo ambalo halionyesha haki kwa upande wa utetezi katika kesi hiyo ambayo uamuzi wake utatolewa Agosti 20,” akasema Bw Ochiel.

Wakili huyo aliongeza kuwa tume hiyo inaweza kushtakiwa kwa kudharau agizo la mahakama.

Kauli hiyo pia ilitolewa na wakili Elias Mutuma ambaye aliwakilisha chama cha Thirdway Alliance katika kesi yake kupinga mswada wa BBI katika mahakama kuu.

“Hatua hiyo ya kutangaza zabuni ni ukiukaji wa wazi wa agizo la mahakama. Hii ni licha ya kwamba IEBC inawajibu waa kuheshimu Katiba hii ambayo inahimiza kuheshimiwa kwa maagizo ya mahakama,” akasema Bw Mutuma.

Lakini kaimu mkurugenzi mkuu wa tume hiyo Hussein Marjan alitetea hatua hiyo ya IEBC ya kutangaza zabuni za ununuzi bidhaa za kura ya maamuzi na uchaguzi, akisema ni sehemu tu ya maandalizi ya tume hiyo.

“Zabuni hiyo inalenga kupata mchapishaji atakayefanya kazi na IEBC katika miaka mitatu ijayo. Tunataka mchapishaji ambaye atatuchapia na kutuwasilishia bidhaa za uchaguzi hitaji likitokea ndani ya kipindi hicho,” Bw Marjan akanukuliwa akisema.

Katika bajeti ya mwaka wa kifedha wa 2021/2022 iliyosomwa bungeni Juni 13, mwaka huu, IEBC imetengewa Sh15 bilioni za kufadhili maandalizi ya uchaguzi mkuu. Hazina ya Kitaifa haikutenga fedha zozote kwa ajili ya kura ya maamuzi.

Mnamo Julai 1, 2021 Shirika la Trend and Insights For Afrika (TIFA) lilitangaza matokeo ya kura ya maamuzi yaliyoonyesha kuwa mchakato wa BBI sio maarufu miongoni mwa Wakenya.

Kulingana na matokeo hayo, ni asilimia 19 pekee na Wakenya waliohojiwa waliosema kuwa wako tayari kushiriki katika kura ya maamuzi na kupiga kura ya “NDIO”.

Kulingana na matokeo hayo, asilimia 31 ya waliohijiwa walisema kuwa watapiga kura ya “LA” endapo shughuli hiyo ingefanyika wakati huo, Juni 20 hadi Juni 30, 2021, utafiti huo ulipoendeshwa.

You can share this post!

Jinsi ya kuandaa meatballs

AU yakashifu ghasia Afrika Kusini, watu 72 wakiuawa