• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 11:42 PM
Babu, 93 ashinda vijana kwa mistari, aoa mke wa umri wa miaka 19

Babu, 93 ashinda vijana kwa mistari, aoa mke wa umri wa miaka 19

Na STEPHEN ODUOR

MWANADADA mwenye umri wa miaka 19, ameshangaza wanakijiji wa Mataarba, kaunti ndogo ya Tana Delta baada ya kuamua kuolewa na babu wa umri wa miaka 93 kwa hiari yake mwenyewe.

Hawaa Roble alifunga pingu za maisha na mzee Abdullah Gardale katika harusi ya kitamaduni iliyofanyika Jumanne.

Licha ya ndoa hiyo kukosolewa na wanakijiji wengi kutokana na tofauti ya umri wa wawili hao, Bi Roble alisema aliamua kuolewa na mzee anayeelewa kutunza mke huku akidai kuwa vijana rika zake hawatoshi mboga.

“Rika zangu ni waoga na hawajali hisia za wengine. Huwa ni vigumu sana kuelewana na mwanamume wa rika yangu ikilinganishwa na jinsi ninavyoelewana na mwanamume mzee,” akasema katika mahojiano na Taifa Leo.

Wawili hao walikutana Kipini ambapo Bi Roble alikuwa akifanya vibarua.

Wakati huo, alikuwa na umri wa miaka 18 na alikuwa amechumbiana na kijana ambaye alitoweka ghafla.

Bi Roble anasema alisubiri kwa muda mrefu kijana huyo arudi ili waoane, lakini akachoka kumngoja.

“Hakutoa sababu yoyote ya kutoroka, wala hakuniaga. Alitoweka tu na nikasikia uvumi kuwa alionekana katika maeneo mengine lakini sijawahi kumwona hadi leo na familia yake pia haijawahi kufichua aliko,” akasema.

Mzee Gardale alianza kumtongoza, na Hawaa akaitikia maneno yake.

Watu wachache waliogundua kuhusu uhusiano wao mapema walijaribu kumkanya, hadi jamaa za mwanamke huyo wakaanza kumgombeza mzee huyo wakimtaka aachane na binti yao.

“Wajomba wangu wengi na hata kaka zangu hawakupendezwa na uhusiano huu lakini mimi nilikuwa nimeridhishwa. Kwa mara ya kwanza nilihisi kupendwa,” akasema.

Jamaa zake waliamini kuwa Bw Gardale alikuwa mzee kupita kiasi na hangetimiza mahitaji ya kihisia ya msichana wa miaka 19.

Walidai kuwa, mwanamume huyo hakufaa kwa sababu aliwahi kutaliki wake zake wawili, na wengine wawili walikuwa wamefariki kwa hivyo hangeishi sana na binti yao.

“Mume wangu ana hekima na nguvu. Wale wanaodhani hana thamani waniulize mimi. Mimi ndiye mke wake, namfahamu ndani na nje,” akasema.

Kwa upande wake, Bw Gardale alisema wanaomkashifu wako huru kufanya hivyo lakini cha muhimu ni kwamba yeye binafsi ana furaha maishani.

“Nimekosolewa na wengi lakini wana haki kutoa maoni yao sawa na jinsi sisi tuna haki ya kuishi kwa furaha,” akasema.

Wawili hao walikuwa wamehamia Malindi kwa muda ili kuepukana na pingamizi hizo.

Jamaa zao walipoona kuwa hawatashinda katika vita hivyo, waliamua kuwaacha wawili hao wafanye watakavyo ndipo wakafunga ndoa Julai 12.

You can share this post!

‘Jinsi Sharon alivyosafirishwa kuuawa’

Wanavoliboli ya ufukweni Kenya kutumia ndege ya Ethiopia...