• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:38 AM
Biden aipapura Facebook kutozima habari za uongo kuhusu corona

Biden aipapura Facebook kutozima habari za uongo kuhusu corona

Na AFP

WASHINGTON DC, Amerika

RAIS wa Amerika, Joe Biden ameonya kwamba uenezaji wa habari za uongo kupitia mitandaoni hasa Facebook kuhusu virusi vya corona ndio umechangia kwa vifo vya watu wengi ulimwenguni.

Tangu aingie mamlakani, Rais Biden amekuwa akipiga vita vikali habari feki kuhusu janga la corona kupitia Facebook huku Marekani ikiendelea kuwapa raia wake chanjo ya kuzuia maambukizi ya virusi hivyo.

“Wanawaua raia. Janga pekee ambalo tuko nalo ni kuhakikisha kuwa watu wote wanapokea chanjo,” akasema.

Uhasama kati ya Facebook na Rais Biden haujaanza leo. Mnamo Januari mwaka jana akilenga kuwania urais, alinukuliwa na jarida la New York Times akisema mmiliki wa Facebook, Mark Zuckerberg ana tatizo kubwa hasa kuwa kuruhusu kuchapishwa kwa taarifa za kumchafulia jina.

Maafisa wa kitengo cha afya nchini Marekani tayari wameonya kwamba kupanda kwa vifo na maambukizi ya corona, kunawaathiri hasa watu ambao bado hawajapokea chanjo ya corona.

Mapema Ijumaa, Mkuu wa Mawasiliano katika ikulu ya White House, Jen Psaki alisema Facebook na mitandao mingine ya kijamii haijafanya juhudi za kutosha kupigana na habari potovu kuhusu chanjo zinazotolewa za corona.

“Japo wamechukua hatua kupigana na ueneaji wa habari potovu kuhusu corona na chanjo, kuna mambo mengi ambayo bado yanahitaji kutekelezwa na Facebook kuzuia tabia hiyo,” akasema Psaki.

Hata hivyo, msemaji wa Facebook Kevin McAlister amekashifu Rais Biden kwa matamshi yake, akisema kampuni hiyo haitayumbishwa katika utendakazi wake na madai ambayo hayana msingi wowote kutoka Marekani.

“Kama kampuni tuliondoa habari feki milioni 18 zinazohusiana na janga la corona. Pia tumekuwa tukidhibiti na kufuta akaunti za watu binafsi au mashirika ambayo yanakiuka kanuni na kueneza uongo kuhusu janga la corona,” ikasema taarifa ya Facebook.

Mtandao wa Facebook umekashifiwa kwa kutofuta machapisho ambayo yana jumbe potovu kuhusu janga la corona.

Jumbe hizo bado zimekuwa zikisambazwa, hali ambayo imetia doa uwajibikaji wa kampuni hiyo na kuikasirisha Marekani. Ijumaa, Mkurugenzi wa Kituo cha Afya cha Kupambana na Kuzuia Magonjwa Marekani, Rochelle Walensky aliwatahadharisha raia ambao bado wamekataa kupokea chanjo kuwa afya yao iko hatarini na kuwashauri wabadili mtazamo.

Ni asilimia 67.9 pekee ya Wamarekani ambao wamepokea dozi ya kwanza ya chanjo huku asilimia 59.7 wakiwa wamechanjwa mara mbili jinsi inavyohitajika. Wengi bado wamekataa kupokea chanjo wakisema hawaiamini na huenda ikawaathiri kiafya.

Mbali na Facebook, mtandao wa YouTube pia umekashifiwa kwa kueneza habari hizo za uongo.

You can share this post!

Mswada bungeni kubuni ‘mwakilishi-wazee’

Wazee wa Kaya watakasa barabara