• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 10:55 AM
Mwigizaji anayepania kutinga upeo wa kimataifa

Mwigizaji anayepania kutinga upeo wa kimataifa

Na JOHN KIMWERE

ANAAMINI anatosha mboga kufanya vizuri katika tasnia ya maigizo na kutinga upeo wa kimataifa miaka ijayo.

Anasema kuanzia mwaka ujao amepania kujituma mithili ya mchwa anakolenga kutimiza ndoto yake katika tasnia ya maigizo wala hatokubali chochote kuzima azma yake.Zuhura Wambui Kinyanjui ambaye kwa jina la utani anafahamika kama Zuchiee ni msanii anayekuja anayelenga kufanya makubwa katika sekta ya uigizaji.

Binti huyu amehitimu kwa shahada ya digrii katika masuala ya maigizo kutoka Chuo Kikuu cha Kenyatta (KU). Kando na uigizaji kisura huyu ni mwandishi wa Script pia analenga kuandika na kuchapisha kitabu chake kabla hajatinga miaka 30. Pia anamiliki chaneli inayoangazia masuala ya kutalii maeneo tofauti iitwayo Zuhura Kinyanjui kwenye mtandao wa YouTube.

ANNE HATHAWAY

”Nilivutiwa na masuala ya sanaa tangia nikisoma shule ya msingi,” anasema na kuongeza kuwa kama ajira alianza kujituma katika maigizo mwaka 2019. Anasema kuwa alivutiwa na uigizaji baada ya kutazama kazi za msanii mahiri kama Anne Hathaway mzawa wa Marekani aliyeshiriki filamu kama ‘Les Miserables’ anayosema kuwa ilimtia motisha zaidi.

Kando na kuwa alihisi angeibuka mwimbaji, mwigizaji na mcheza densi tangia akiwa mtoto alitamani sana kuhitimu kuwa daktari ama mwana habari wa televisheni. Chipukizi huyu anasema anashiriki uigizaji akifuata nyayo zake msanii shupavu Jennifer Joanna Aniston mzawa Marekani aliyeshiriki filamu kama ‘Murder Mystery,’ ‘Just go with it,’ na ‘Friends,’ kati ya zingine.

Picha/JOHN KIMWERE
Msanii anayekuja Zuhura Wambui Kinyanjui maarufu Zuchiee.

Dada huyu ameshiriki filamu kadhaa chini ya makundi tofauti ndani ya miaka miwili iliyopita. Chini ya Anga Creations ameshiriki filamu mbili ‘Wingu,’ na ‘Ella.’ Pia kupitia IBON Entertainment amecheza filamu ya stage play iitwayo Murder Most Scandalous.

MWIGIZAJI WA KIKE BORA

Anajivunia kushiriki filamu kwa jina ‘The Runaway,’ anayosema ilimpatia changamoto kubwa wakati walipokuwa wakiitengeneza. ”Ninashukuru Mola maana filamu hiyo ilipata mpenyo na kupeperushwa kupitia runinga ya KuTV,” akasema na kutaja kuwa filamu hiyo ilimhitaji ajitolee kwa ukakamavu wa hali ya juu maana iliangazia suala la utumwa wa ngono.

Filamu hiyo ilichangia chipukizi huyu kupokea tuzo ya mwigizaji bora wa kike mwaka 2018.Anasema barani Afrika angependa kufanya kazi na mwigizaji wa filamu za Kinigeria ‘Nollywood’ Genevieve Nnaji anayejivunia kufanya kazi nzuri kama ‘Blood Sister,’ na ‘Power of Love,’ kati ya zingine.

”Bila kuweka katika kaburi la sahau filamu hizo zilipata umaarufu hapa nchini nikiwa mtoto,” akasema.Pia angefurahi kujikuta jukwaa moja na msanii mahiri, Lesley-Ann Brandt mzawa wa Afrika Kusini.

Binti huyu anasema serikali inastahili kutenga fedha za kupiga jeki sekta ya uigizaji kwa kuzipigia debe kazi zinazozalishwa humu nchini. Msichana huyu aliyezaliwa mwaka 1995 anashauri wenzie kuwa mwigizaji sio jambo rahisi lazima wawe na mwito pia wajitume kiume bila kulegeza uzi.

Akijibu swali kuhusu kilichowahi mfanya alie katika mahusiano alisema hata jambo ndogo huvuruga wapendanao. Alidokeza kuwa aliwahi kumwaga machozi mpenziwe alipodinda kupokea simu yake.

  • Tags

You can share this post!

Mwana habari na mwigizaji chipukizi anayepania kuzidisha...

SONIA: Chipukizi anayelenga nyayo za Priyank Chopra