• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 9:50 AM
Sancho sasa atambulishwa kwa mashabiki

Sancho sasa atambulishwa kwa mashabiki

Na MASHIRIKA

FOWADI Jadon Sancho amesema kujiunga kwake na Manchester United “ni kujibiwa kwa ndoto yake kitaaluma”.

Nyota huyo raia wa Uingereza amerasimisha uhamisho wake kutoka Borussia Dortmund hadi Manchester United kwa kima cha Sh11.3 bilioni.

Anakuwa mchezaji wa pili ghali zaidi kutoka Uingereza ambaye amewahi kusajiliwa na Man-United baada ya beki na nahodha Harry Maguire aliyetokea Leicester City mwishoni mwa 2018-19.

Sancho pia ndiye mchezaji wa pili ghali zaidi kuwahi kutua Old Trafford baada ya kiungo Paul Pogba kusajiliwa na Man-United kwa kima cha Sh12.4 bilioni kutoka Juventus mnamo 2016.

Chini ya kocha Ole Gunnar Solskjaer ambaye ni raia wa Norway, Man-United waliweka mezani kima cha Sh11.2 bilioni ili kumshawishi Maguire kuagana na Leicester.

Licha ya kufuzu kwa kipute cha Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo 2021-22, Dortmund walikuwa na ulazima wa kuagana na baadhi ya wanasoka wao wa haiba kubwa msimu huu ili kupunguza gharama ya matumizi kutokana na athari za janga la corona.

Ili kuzamisha maazimio ya Man-City na Chelsea kuendelea kumfukuzia Haaland, Dortmund wamefichua kwamba bei mpya ya fowadi huyo wa zamani wa RB Salzburg nchini Austria ni Sh19.6 bilioni. Man-City waliokuwa waajiri wa zamani wa Sancho sasa watatia kapuni bonasi ya Sh1.5 bilioni baada ya Sancho kufanikisha uhamisho wake hadi Man-United.

Sancho alianza kusakata soka ya kulipwa ugani Etihad na alikataa ofa mpya ya Sh4.2 milioni kwa wiki na kuhiari kuyoyomea Ujerumani akiwa na umri wa miaka 17. Hofu yake ilikuwa ni kukosa uhakika wa kuunga kikosi cha kwanza cha Man-City chini ya kocha Pep Guardiola aliyekuwa ametokea Bayern Munich wakati huo.

Kufikia sasa, Sancho amfungia Dortmund mabao 50 kutokana na jumla ya mechi 137. Anajivunia kufungia timu ya taifa ya Uingereza jumla ya mabao matatu kutokana na mechi 18.

Nyota huyo aliyezaliwa katika eneo la Camberwell, Kusini mwa jiji la London, alijiunga na akademia ya Watford akiwa na umri wa miaka saba kabla ya Man-City kumsajili kwa Sh9.2 milioni pekee akiwa na umri wa miaka 14. Uhamisho wake hadi Dortmund ulishuhudia Watford wakipokezwa na Man-City kima cha Sh70 milioni zaidi.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Kocha wa ndondi adai Okoth alishinda

360 Media yatua kileleni, Makarios, Leopards zikiteleza