• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 2:07 PM
Polisi wadaiwa kurusha kilipuzi katika baa

Polisi wadaiwa kurusha kilipuzi katika baa

Na WAWERU WAIRIMU

POLISI wamehusishwa na mlipuko uliofanyika katika baa moja mjini Isiolo mnamo Jumanne alfajiri huku habari mpyazikiashiria kuwa kilipuzi hicho kilirushwa na afisa wa polisi.

Imebainika kuwa kisa hicho ambapo mwanaburudani mmoja alijeruhiwa hadi nyeti zake zikakatika, huenda hakikusababishwa na jaribio la kulipiza kisasi katika mgogoro wa kimapenzi.

Ripoti za awali ziliashiria kuwa mshukiwa anayesemekana kuwa afisa wa polisi, alikuwa anamlenga kwa kilipuzi hicho, mwanamke waliyetengana naye miezi mitatu iliyopita.

Hata hivyo, kilimwangukia mtu mwingine aliyekuwa kilabuni humo na kulipuka alipokuwa amekishikilia kwa nguvu ili kisianguke kwenye sakafu.

Wafanyakazi katika baa hiyo ya Genesis Pub, ambayo sasa ni eneo la uhalifu, walidai kuwa kilipuzi hicho kilirushwa katika baa hiyo na wanaume waliovaa magwanda ambao walikuwa wakipiga doria usiku wa tukio hilo.

Baa hiyo ilikuwa ikiendesha shughuli zake wakati wa saa za kafyu japo maafisa hawajamkamata mtu yeyote akiwemo mmiliki wa kilabu hicho kwa kukiuka sheria hizo za Covid-19.

Aidha, wafanyakazi hao walidai kuwa kabla ya kisa hicho kutokea, baadhi ya maafisa wa polisi walizuru jengo hilo na kumwamrisha mhudumu wa kike aliyekuwa kwenye kaunta, kuwaruhusu waingie la sivyo wangejutia.

“Aliwaeleza (maafisa) kwamba hakuwa na funguo za lango kuu. Waliingia kwa kutumia mlango wa chumba jirani cha kibiashara lakini akawasihi wasubiri huku akisaka funguo,” mfanyakazi mmoja alieleza Taifa Leo.

Karibu dakika mbili baadaye, huku wakiwa wamechoka kusubiri na wakiwa wameghadhabika, afisa mmoja anadaiwa kurusha kilipuzi ndani ya kilabu hicho ambapo watu kadhaa walikuwa wameketi wakijiburudisha kwa vinywaji, mfanyakazi mwingine alisema.

“Kifaa hicho kilikuwa na nguvu nyingi. Jengo lote lilitikisika, likapasuka na vifusi kuporomoka huku likimwangukia mwanaburudani mmoja na kunyofoa nyeti zake na kujeruhi miguu yake.

“Mali nyingineyo katika jengo hilo ikiwemo friji na vileo pia iliharibiwa,” alisema.

Pamoja na timu hiyo ya maafisa wa polisi, ambayo gari lao lilionekana likiwa limeegeshwa nje ya baa jirani, alikuwemo afisa mkuu wa polisi ambaye wengi waliozungumza, walisema wanamjua vyema.

Bado haijabainika ni wapi mshukiwa huyo, ambaye angali mafichoni, alitoa kilipuzi hicho.

Huku polisi wakichelea kuzungumza kuhusu wanachokifahamu na kusisitiza kwamba uchunguzi unaoendelea utasaidia tu kubaini kilichotokea kabla na wakati wa tukio hilo, Taifa Leo imefichua kwamba makachero wamekuwa wakijikuna kichwa kutegua kitendawili hicho.

You can share this post!

Naomi Osaka aingia raundi ya tatu ya tenisi ya mchezaji...

Familia yaahirisha mazishi ya Kangogo