• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
Tumaini shirika la Ubelgiji likifadhili uchimbaji kisima eneobunge la Ganze

Tumaini shirika la Ubelgiji likifadhili uchimbaji kisima eneobunge la Ganze

Na ALEX KALAMA

WAKAZI wa eneo la Kavunzoni, Kaunti ya Kilifi wana matumaini kwamba tatizo la uhaba wa maji ambalo limewakumba kwa miaka mingi litatatuliwa hivi karibuni.

Hii ni baada ya shirika la kutoka Ubelgiji kufadhili uchimbaji wa kisima katika eneo hilo lililo eneobunge la Ganze.

Wakiongozwa na Bw Robert Chengo, wakazi hao hata hivyo wameitaka serikali ya kaunti hiyo kuwasambazia wakazi maji wanaposubiri kisima hicho kukamilika.

“Hiki kisima kitasaidia wakazi wote wa Goshi na eneo la Mitangani. Huwa tunatoka hapa asubuhi saa moja tukifika mahali pa kuchota maji ni saa tano, kisha kurudi hapa ni saa nane au saa tisa ndipo tunashukisha maji,” akasema Bw Chengo.

Kulingana na mbunge wa eneo hilo Teddy Mwambire, serikali ya Kaunti ya Kilifi inafaa kushirikiana na mashirika mbali mbali ili kuhakikisha eneo hilo linapata maji.

“Hii sehemu ya Kavunzoni, Goshi kuenda mpaka karibu na Mnagoni imekuwa kame na maji unapata baada ya kutembea kilomita takribani 20. Mtungi mmoja ule wa lita 20 wanauziwa kwa Sh50. Ushirikiano utasaidia kuhakikisha kwamba hili eneo linapata maji kwa haraka,” alisema Bw Mwambire.

Wakazi wa eneo hilo waliupongeza ufadhili huo wakisema utawapunguzia changamoto ya kutembea mwendo mrefu kutafuta maji.

You can share this post!

SGR, barabara nzuri ndiyo rekodi kuu ya Uhuru –...

Zogo lakumba fidia ya wavuvi Lamu