• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
Covid-19: UN yarai mataifa kuanza kufungua shule zao

Covid-19: UN yarai mataifa kuanza kufungua shule zao

Na AFP

GENEVA, Uswisi

UMOJA wa Mataifa (UN) umezirai nchi ambazo bado zinaendelea kufunga shule kutokana na janga la virusi vya corona kuzifungua, ili kuwaruhusu wanafunzi kurejelea masomo yao.

Umoja huo ulisema kuwa hali hiyo inawaathiri zaidi ya watoto 600 milioni kote duniani, ikivuruga pakubwa mpangilio wa masomo yao.

“Hali haiwezi kuendelea namna hii,” akaeleza James Elder, ambaye ndiye msemaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Maslahi ya Watoto (UNICEF) kwenye kikao na wahahabari jijini Geneva, Uswisi.

Ingawa alikubali nchi nyingi zinakabiliwa na wakati mgumu kufanya maamuzi kuhusu njia za kukabili janga hilo, alieleza “shule zinapaswa kuwa taasisi za mwisho kufungwa na za kwanza kufunguliwa.”

Alisema ni makosa kwa nchi kufungua upya baa na vituo vya burudani kabla ya kufungua shule.

“Si lazima walimu na wanafunzi wote kupewa chanjo ndipo shule ziweze kufunguliwa,” akasema.

Alizirai nchi kutopunguza fedha zinazoitengea sekta ya elimu licha ya changamoto za kiuchumi zilizosababishwa na janga hilo.

Barani Ulaya, wanafunzi wengi wako likizoni. Hata hivyo, inakisiwa kuwa karibu nusu ya wanafunzi wote katika maeneo ya mashariki na kusini mwa Afrika wamo majumbani mwao kutokana na athari za janga hilo.

Kijumla, zaidi ya watoto 32 milioni wanakisiwa kuwa nyumbani katika maeneo hayo baada ya shule kufungwa kutokana na athari zinazohusiana na janga hilo.

Nchi nyingi zimekuwa zikilazimika kufunga shule mara tu baada ya kiwango cha maambukizi kuanza kuongezeka.

Hilo linaifanya hali hiyo kudorora kwani kabla ya janga kutokea, ilikisiwa watoto karibu 37 milioni hawakuwa wakienda shuleni licha ya kufikisha umri unaohitajika.

Katika bara Asia na eneo la Pacific, shule katika eneo hilo zimefungwa kwa zaidi ya siku 200 kutokana na janga hilo.

Katika eneo la Amerika Kusini na Carribean, nchi 18 zimefunga shule zake ili kudhibiti maambukizi ya virusi hivyo.

“Kutokana na hali hiyo, nchi sasa zimelazimika kukabili visa vya ghasia za kinyumbani, hali ya wasiwasi na ongezeko la mimba za mapema miongoni mwa wasichana,” akasema Elder.

Alitoa mfano wa Uganda, ambapo kati ya Machi 2020 na Juni 2021, taifa hilo lilirekodi ongezeko la karibu thuluthi moja ya mimba za mapema miongoni mwa wasichana walio kati ya umri wa miaka 10 na 24. Kulingana na shirika hilo, idadi kubwa ya wanafunzi hawawezi kumudu gharama za kushiriki masomo kwa njia ya mtandao.

You can share this post!

Ni wale wale wa ahadi hewa 2022

MAKALA MAALUM: Wakazi Limuru katika njiapanda kuhusu...