• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:39 PM
CHOCHEO: Usiwe mwepesi wa kumeza chambo

CHOCHEO: Usiwe mwepesi wa kumeza chambo

Na BENSON MATHEKA

“NIMEANGUKIA, Mike ana kila kitu nilichotamani kwa mchumba wa maisha yangu,” Lena alikumbuka Brigitte akimwambia alipompata Mike.

Hii ilikuwa miaka minne iliyopita na juzi alijipata akimfariji rafiki yake ambaye amepitia maisha magumu katika ndoa yake na Mike.

“Nimejifunza kitu kimoja muhimu katika uhusiano wa Brigitte na Mike; usishawishike haraka na mistari ya mwanamume. Hiyo mistari mitamu na chambo anachokurushia haziakisi hali halisi ya tabia yake au maisha ya baadaye mtakayokuwa nayo,” asema Lena.

Mwanadada huyu anakumbuka kwamba Brigitte alikataa ushauri wake na hata wa wazazi wake waliomtaka achukue muda kufahamu tabia za Mike.

“Alikuwa amepagawishwa na mwanamume huyo. Alikataa ushauri wa marafiki, pasta na wazazi wake waliomtaka asimchangamkie Mike kabla ya kumfahamu vyema. Nafikiri ni magari na utanashati wa mwanamume huyo uliomuingiza boksi haraka. Pili, Mike alikuwa akimpeleka kujivinjari nje ya nchi jambo ambalo wachumba wetu hawakuweza kutufanyia. Brigitte alijiona amefaulu tofauti na sisi ambao wapenzi wetu hawakuweza kumudu maisha ya anasa,” asema Lena.

Kulingana na Seth Kamau, mtaalamu wa masuala ya mahusiano wa kituo cha Abundant Love Care jijini Nairobi, watu wanaoshawishika haraka na mistari ya mapenzi huwa katika hatari ya kutumbukia katika majuto baadaye.

“Nyuma ya hiyo mistari mitamu kunaweza kuwa uchungu usioweza kumezeka. Nyuma ya kinachokuvutia kwa mtu kunaweza kuwa na hatari kubwa. Hivyo basi, kabla ya kumeza chambo, kuwa makini kwa kuwa kinaweza kuwa na sumu,” asema Seth.

Anasema watu wengi huwa wanakosa au kupuuza ushauri kuhusu wachumba walio na mistari mitamu wakishawishika kuwa wamepata waliotamani.

“Kuna wanaoshawishika haraka, wanafunga ndoa wakifikiri watakuwa na maisha ya raha kisha wanajipata katika balaa. Wengi wanagundua kuwa waliodhani ni malaika ni sawa na ibilisi wanaowatesa. Ule utamu uliokuwa kwenye mistari unakosekana na kuwa kilio,” asema.

Kulingana na Pasta Patrick Kweyu wa kanisa la Souls Paradise, Nairobi ambaye amekuwa akishauri maharusi, mistari ya mapenzi huwa inanuiwa kuingiza mtu boksi pekee na wala haifai kuchukuliwa kama hali halisi ya maisha ya ndoa.

“Mtu akikuingiza boksi halafu atake kukuoa mara moja, usikubali. Chukua muda umfahamu vyema, hasa tabia zake. Usiamini chochote anachokuambia au usipagawishwe na anachokufanyia kabla ya kupata ukweli. Mazuri hayo yanaweza kuwa ya kuficha tabia zake mbovu. Chukua hatua wewe binafsi pasipo pupa umdadisi, tena kwa kina kabla ya kukata kauli kufunga naye pingu za maisha. Hii haraka ambayo watu huwa nayo kwa sababu ya utamu wa mistari ya mapenzi au zawadi za hapa na pale, haina baraka,” asema Kweyu.

Seth na Kweyu wanakubaliana kuwa misitari ya mapenzi hunuiwa kutimiza ajenda ya muda mfupi na haifai kuchukuliwa kama hali halisi ya maisha ya ndoa.

“Wanachokosa kufahamu watu wengi ni kuwa maneno matamu ambayo wapenzi hubadilishana huwa ya kutimiza malengo ya muda mfupi. Kwa mfano, mwanamume anaweza kutaka mrembo akatae wanaume wengine ampende yeye au nia iwe ni kuchovya asali tu. Mwanadada anaweza kumweleza mwanamume maneno ya kutoa nyoka pangoni lakini awe na lengo tofauti na uhusiano wa muda mrefu,” aeleza Seth.

Hata hivyo, wataalamu wanasema maneno matamu yanayoambatana na tabia nzuri, ukweli na vitendo, heshima na nidhamu yanaweza kuwa hakikisho ya maisha ya raha siku za baadaye.

“Hii ni pale tu watu wanapoendelea kubadilishana mistari hata baada ya kuwa kwenye uhusiano kwa muda na hata baada ya kuoana. Ikikatika baada ya kuingia boksi, elewa kwamba mambo sio mazuri, jiandae kwa balaa,” asema Kweyu.

You can share this post!

FUNGUKA: ‘Haja yangu pesa tu!’

Mbinu za kuzima Ruto Mlimani zaanza kusukwa