• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 5:22 PM
FAUSTINE NGILA: Tuna kibarua kukuza miji ya kibiashara na kiteknolojia

FAUSTINE NGILA: Tuna kibarua kukuza miji ya kibiashara na kiteknolojia

Na FAUSTINE NGILA

SUALA muhimu lililojitokeza katika ziara ya Rais Uhuru Kenyatta nchini Uingereza wiki iliyopita, lilikuwa azma ya kufanya Nairobi kuwa jiji la kibiashara kimataifa.

Ilitangazwa pia kuwa kama kituo cha biashara barani Afrika, Nairobi ingetia saini mkataba mwingine na jiji la London, Uingereza, kuwezesha Kenya kujifunza mengi kuhusu usimamizi wa miji ya kibiashara.

Lakini kama tunavyojua, tumekuwa na mipango ya kuanzisha kituo kama hicho tangu Bunge lipitishe Sheria ya Kituo cha Biashara ya Kimataifa cha Nairobi mnamo 2007. Kwenye tovuti yake, kituo hicho kinafaa kuzinduliwa rasmi mwishoni mwa mwaka huu.

Lakini sioni hilo likifanyika.Sababu kuu ni kwamba hatujaweka miundomsingi ifaayo kwa kituo kama hicho.

Ukitazama kote duniani, miji ya kibiashara imekuwa ikijengwa mahali kuna mabenki, kampuni za ufadhili wa kifedha na masoko ya hisa.Itatubidi tuwekeze pakubwa katika sekta ya ujenzi na uuzaji wa majumba na maeneo makubwa, ili kutimiza azma yetu ya kujenga kituo hicho.

Rwanda, kwa mfano, imechukua mtindo huo. Mwaka uliopita, Rwanda ilipatia benki ya Equity – ya kutoka humu nchini – kandarasi ya kujenga jumba la Kigali Financial Tower ambapo kutakuwa na Kituo Cha Kimataifa cha Fedha cha Kigali.

Hapa kwetu, tumeanza vibaya kwani tayari hatuna eneo maalum ambako tunaweza kujenga kituo cha kimataifa cha kibiashara.Hii ni licha ya serikali kusema kuwa, mwekezaji yeyote ameruhusiwa kujenga kituo kama hicho popote nchini baada ya kupewa leseni.

Dunia ya sasa pia imetufundisha kwamba wawekezaji huvutiwa na mji wa kibiashara iwapo tayari kuna shirika la serikali la kutangaza, kuendeleza na kusimamia mji huo; pamoja na kuwa na kampuni ya kutoa leseni kwa biashara zote zilizo humo.

Pili, tunahitaji halmashauri huru ya kusimamia na kudhibiti wafanyabiashara wote katika eneo hilo maalum la kiuchumi.

Jijini Dubai, gavana wa benki kuu ndiye pia mwenyekiti wa Kituo cha Kimataifa cha Kifedha cha Dubai.Badala ya halmashauri kama hii, tulicho nacho kwa sasa ni kamati iliyojaa wanasiasa, wasioelewa jinsi kituo kama hiki kinafaa kuendeshwa.

Pia kunahitajika mahakama maalumu ya kutatua migogoro ya kibiashara miongoni mwa wawekezaji katika mji huo, ikitilia maanani sheria za kimataifa.

Upo wakati ambapo Wizara ya Fedha ilishirikiana na Mamlaka ya Usimamizi wa Viwanja vya Ndege kutoa ardhi ambapo kituo hicho cha biashara ya kimataifa kinafaa kujengwa, lakini juhudi hizo sasa zinafaa kufuata mwongozo wa miji mingine ya kimataifa duniani Singapore na Hong Kong.

Ili kuvutia zaidi wawekezaji tutahitaji kumiliki asilimia 100 ya kampuni zinazokuja, na vile vile kuondoa ushuru mwingi unaotozwa kampuni za Kenya kwa sasa.

Kwa kuendelea kufanya utafiti kuhusu vituo vya kibiashara duniani, huenda tukajijengea kituo bora zaidi hapa Afrika.

Lakini iwapo tutashikilia mkondo tunaofuata kwa sasa, huenda mradi huu ukasambaratika kwa kujenga vitu vinavyofukuza wawekezaji.

Pia mradi unaweza kuishia kukwama kama ule wa Konza TechnoCity. Lazima tuwe makini sana.

You can share this post!

UDA ni chama cha mahasla – Ruto

CHARLES WASONGA: Tukatae mswada wa kulipia wabunge bima ya...