Na CHARLES WASONGA
SHIRIKA la Utabiri wa Hali ya Anga limeonya kuwa hali ya kiangazi itashuhudiwa maeneo kadha nchini huku likiongeza kuwa hali hiyo itaandamana na njaa, ukosefu wa maji na lishe ya mifugo.
Katika utabiri wake wa hivi punde, shirika hilo pia linasema msimu wa baridi unaoshuhudiwa katika maeneo ya Nairobi na Bonde la Ufa utafikia kikomo mwezi huu.
Kwenye taarifa aliyoitoa Jumanne, mkurugenzi mkuu wa shirika hilo Stella Aura alisema maeneo hayo mawili yatashuhudia kiwango cha joto cha nyuzijoto 26 hadi 28, kwa wastani.
“Hata hivyo, maeneo mengine ya nchi yataendelea kushuhudia hali ya jua na anga kavu,” akaeleza.
“Msimu wa baridi unakamilika mwezi wa Agosti haswa katika nyanda za juu mashariki mwa Rift Valley (ikiwemo kaunti ya Nairobi),” Bi Aura akaongeza.
Utabiri wa mwezi wa Agosti pia unaonyesha kuwa maeneo karibu na Ziwa Victoria, Magharibi mwa Rift Valley, Kati mwa Nchi, Kusini mwa Rift Valley na maeneo ya Kaskazini Mashariki mwa Kenya yatapata kiangazi.
Hali ya joto inatarajiwa kushuhudiwa katika ukanda wa pwani, nyanda za chini za mashariki mwa Kenya na Kaskazini Mashariki mwa Kenya katika mwezi huu wa Agosti.
Hata hivyo, Bi Aura alisema mvua chache itashuhudiwa katika maeneo fulani ya Rift Valley na hivyo kutoa hali bora kwa shughuli za kilimo.
“Kwa upande mwingine, hali ya jua kali na joto katika maeneo ya kaskazini mashariki na kaskazini magharibi mwa Kenya na kusini mwa Kenya italeta upungufu wa lishe ya mifugo na maji kwa matumizi ya binadamu na mifugo,” akaeleza.
Alisema serikali inafaa kuweka mikakati ya kupunguza makali ya kiangazi katika maeneo hayo ya kaskazini mwa Kenya “ili kuzuia hasara kutokana na vifo vya mifugo.”
“Ikiwa hatua za haraka hazitachukuliwa kukabiliana na hali hii, huenda migogoro kati ya wanyama na binadamu ikashuhudiwa katika maeneo hayo kame.”