• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 4:36 PM
Madiwani Kisumu walaumiwa kwa ziara ya Tanzania

Madiwani Kisumu walaumiwa kwa ziara ya Tanzania

Na RUSHDIE OUDIA

MADIWANI wa kaunti ya Kisumu wameshutumiwa vikali kwa kufanya ziara ya wiki moja ya mafunzo nchini Tanzania, ziara ambayo wakazi wanasema haina umuhimu wowote.

Madiwani hao walizuru taifa hilo jirani kujifunza kuhusu uchukuzi ziwani na jinsi wakazi wa Kisumu wanaweza kufaidi kutokana na rasilimali zilizoko Ziwa Victoria.

Wakazi walisema inasikitisha kuwa ziara hiyo ilijiri wakati kaunti ya Kisumu inaathirika na makali ya janga la corona na ukosefu wa fedha.

Japo idadi ya madiwani waliofanya ziara hiyo haijulikani, wakazi walielezea hasira zao kupitia mitandao ya kijamii wakiwasuta viongozi hao kwa kufuja pesa za umma.

Walisema ziara kama hiyo haisaidii kwa njia yoyote katika vita dhidi ya corona, wakisema ndio changamoto inapaswa kupewa kipaumbele.

Madiwani hao na baadhi ya wafanyakazi wa bunge la kaunti ya Kisumu inadaiwa kuwa wiki jana, Julai 26 walielekea Tanzania na kurejea jana baada ya kuzuru miji ya Arusha na Mwanza. Hivi majuzi, wafanyakazi wawili wa bunge hilo walifariki kutokana na ugonjwa wa Covid-19.

Bunge hilo la kaunti ya Kisumu linatarajiwa kujibu malalamishi ya wakazi kupitia taarifa ndefu na maelezo ya kina kuhusu ziara hiyo.

Hata hivyo, madiwani wawili walitetea ziara hiyo wakisema walijifunza mengi kutoka miji hiyo katika taifa jirani tofauti na madai kwamba ziara yao haikuwa na manufaa yoyote.

Diwani wa wadi ya Milimani Market Sethe Adui Kanga na mwenzake wa wadi ya Awasi Onjiko Maurice Ngeta na Stephe Owiti (wadi ya Kolwa Mashariki) walisifu ziara hiyo.

“Ziara hiyo ilikuwa yenye manufaa kwetu. Tunapanga kutekeleza yale ambayo tulijifunza,” akasema Bw Kanga.

You can share this post!

ODM yaponda ‘usuhuba’ wa Ruto, Museveni

WANDERI KAMAU: Tumekisaliti kizazi cha sasa kwa jina la...