• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 12:26 PM
Mtangazaji wa zamani wa KBC Gladys Erude afariki

Mtangazaji wa zamani wa KBC Gladys Erude afariki

Na Derick Luvega

MTANGAZAJI maarufu aliyevuma katika miaka ya 1980 na 1990 Gladys Erude, alifariki Jumatano usiku akiwa na umri wa miaka 70.

Kifo chake kilitokea wiki moja baada ya kurejea nchini kutoka Amerika ambapo amekuwa akitibiwa tangu alipogunduliwa kuwa na saratani mnamo 2019, kulingana na mwanawe, Bw Bonny Erude.

“Amekuwa akiendelea kupata nafuu. Pia alikuwa na matatizo ya moyo. Aliomba kurejea nyumbani (Kenya) ili awaone watu wake. Alikuwa kijijini kwa siku chache na alirejea Nairobi Jumapili,” alisema.

Alifariki nyumbani kwao Nairobi alipokuwa akisubiri ambulensi ya kumkimbiza hospitalini.Kaka yake Laban Kirigano alikuwa wa kwanza kuthibitisha kifo cha dada yake akieleza kwamba alikuwa nyumbani kwao kijijini baada ya kukaa kwa muda mrefu Amerika.

“Ni kweli amekufa. Amekuwa akiishi Amerika ambapo watoto wake wanne wanafanya kazi. Alirejea wiki iliyopita,”alisema Bw Kirigano.

Alipowasili nchini, alitembelea familia yake Vihiga, kisha akamtembelea dadake na hatimaye akaenda nyumbani kwake katika Kaunti ya Nandi.

Katika enzi zake, alivuma kwenye ulingo wa utangazaji kwa miaka 25 katika Idhaa ya Kitaifa (VoK) ambayo sasa inafahamika kama Kenya Broadcasting Corporation (KBC).

Alishinda zimwi la urithi wa wanawake akiwa na umri mchanga wa miaka 24, baada ya kifo cha mume wake Bw Erude, waliyejaaliwa naye watoto sita wa kiume.

Aliwahi kufichua jinsi jamaa zake walivyomgeuka na kuanza kumtesa hali iliyomlazimu kuhama Tigoi, Kaunti ya Vihiga na kwenda Kaunti ya Nandi ambapo alinunua ardhi na kuanza kuishi.

Watoto wake wanne wanafanya kazi Amerika kama daktari wa upasuaji, afisa wa polisi, mhandisi na mtaalam wa mitambo, huku wengine wakiwa mhudumu katika uwanja wa ndege na pasta.

You can share this post!

Aliyemuua Rais Museveni mitandaoni anaswa Uturuki

Uganda yamruka Ruto kuhusu ziara yake iliyotibuka