• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 5:39 PM
Shule yakosa kupata wanafunzi wa kidato cha kwanza

Shule yakosa kupata wanafunzi wa kidato cha kwanza

Na BRIAN OJAMAA

Huku wanafunzi wa kidato cha kwanza wakiendelea kuripoti katika shule walizoitwa, shule moja katika Kaunti ya Bungoma haijasajili hata mwanafunzi mmoja.

Shule ya sekondari ya Mikokwe iliyo Kaunti-ndogo ya Bumula, Bungoma, haijapokea mwanafunzi yeyote wa kidato cha kwanza.

Shule hiyo ilitengewa wanafunzi watatu pekee na Wizara ya Elimu ambao walitarajiwa kujiunga nayo kuanzia Jumatatu.

Hata hivyo, watatu hao hawajaripoti katika shule hiyo ambayo ilianzishwa zaidi ya miaka saba iliyopita.Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Dickens Lumati aliambia Taifa Leo kwamba huenda kutengewa wanafunzi watatu kulitokana na makosa kwa kuwa ina uwezo wa kuwa na wanafunzi wengi.

“Ni wanafunzi watatu pekee waliopewa nafasi katika shule yetu na wote hawajaripoti,” alisema.

Mwalimu huyo mkuu alisema kwamba anahofia huenda shule hiyo haitakuwa na wanafunzi wa kidato cha kwanza mwaka huu.

Alisema mmoja wa wanafunzi watatu waliotakiwa kujiunga na shule hiyo alipewa nafasi hiyo kimakosa kwa kuwa anatoka eneo la Webuye Mashariki ilhali shule ni ya kutwa na iko mbali na nyumbani kwao.

“Sidhani ataripoti. Ni vigumu kuwa na mwanafunzi wa kutwa anayesafiri zaidi ya kilomita 80,” alisema Lumangati.

Alisema shule hiyo ina uwezo wa kuwa na wanafunzi 60 wa kidato cha kwanza lakini kufikia Ijumaa hakuna hata mmoja aliyekuwa ameripoti.Shule hiyo ina walimu sita walioajiriwa na TSC huku wengine wakiwa wameajiriwa na bodi.

Huu ni mwaka wa nne shule hiyo kuwa na watahiniwa katika mtihani wa KSCE.Katibu Mkuu wa tawi la Bungoma Kusini la chama cha walimu Kenya (Knut) Ken Nganga alilaumu mfumo wa Wizara ya Elimu wa kuteua wanafunzi wa kidato cha kwanza akisema unafaa kunyooshwa ili changamoto zilizoshuhudiwa mwaka huu zisirudiwe mwaka ujao.

Alisema mfumo wa zamani ambao wanafunzi walikuwa wakiitwa shule walizochagua unafaa kurudiwa.

Nganga alisema kwamba katika mfumo wa sasa wa kidijitali, wanafunzi wengi waliitwa shule za kutwa za mbali ambazo hawawezi kujiunga nazo.

Alisema baadhi ya wanafunzi waliopata alama nzuri waliitwa katika shule ndogo. Pia, alikosoa kuanzishwa kwa shule bila mpango mzuri.

Shule nyingi zilianzishwa na CDF bila kuzingatia umbali na baadhi ya zilizoko kwa sasa zitakabiliwa na tatizo kama hilo,” alisema.

You can share this post!

Hisia mseto Ezekiel Mutua akitimuliwa kutoka kwa bodi ya...

Wakosoa Magoha kutosajili shule