• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 6:55 PM
Ruto akita kambi Nakuru kupigia debe mfumo wa kumuinua mwananchi wa kipato cha chini

Ruto akita kambi Nakuru kupigia debe mfumo wa kumuinua mwananchi wa kipato cha chini

Na RICHARD MAOSI

NAIBU Rais William Ruto alikita kambi katika eneo la Elementaita, Kaunti ya Nakuru, Jumatatu kupigia debe muundo wa kuimarisha uchumi unaolenga kumtoa mtu wa kipato cha chini katika lindi la umaskini hadi katika viwango vya maisha bora.

Muundo huo anauita ‘bottom -up economy’ na umezua mjadala kote nchini.

Ruto alihudhuria kikao hicho ambacho kiliwaleta pamoja washikadau, wasomi pamoja na viongozi wa kutoka eneo la Nyanza kuzungumzia maswala muhimu ya kiuchumi na biashara.

Akiwahutubia wanahabari, Ruto alieleza kuwa kuna haja ya kuboresha teknolojia ya uzalishaji wa mimea na mifugo, kama nia mojawapo ya kupiga jeki maendeleo.

Aidha aliwashtumu viongozi wanaopinga muundo wa Bottom-Up, akisema wengi wao walikuwa na nia ya kujitengenezea nyadhifa za uongozi.

Ni katika hafla hiyo ambapo washikadau na viongozi waliweka mikakati ya kufanikisha mambo matatu muhimu, katika hatua ya kukwamua raia kutokana na hali ngumu ya maisha, hususan wakati huu taifa likiendelea kupigana na janga la Covid-19.

Alisema kuwa uwekezaji katika sekta ya umma na binafsi utasaidia kuboresha miundomisingi ya nchi na hatimaye kutengeneza nafasi nyingi za ajira miongoni mwa vijana, ikizingatiwa kuwa asilimia kubwa hawana kazi.

Pili alisema kuwa serikali imeanzisha mikakati ya namna ya kuimarisha uzalishaji katika sekta ya kilimo kuanzia miwa, parachichi, ndizi, mahindi na mihogo.

“Ninatumai wale wanaopinga mapendekezo haya wataitikia wito tuandae kikao cha majadiliano ambayo yataleta mapendekezo muhimu kuhusu namna ya kumfaa raia wa kawaida,” akasema.

Aidha aliwataka wakome kuhepa kila mara mjadala kuhusu namna ya kukwamua uchumi wa nchi unapojadiliwa.

You can share this post!

Corona yavuruga mipango ya vikosi siku chache kabla ya...

Kalonzo azindua sekretarieti ya kushirikisha kampeni zake...