• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 8:55 PM
IEBC motoni kuhusu pesa za kampeni

IEBC motoni kuhusu pesa za kampeni

Na WINNIE ONYANDO

WABUNGE Jumatano waliishutumu Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kwa kuchapisha kanuni kuhusu ufadhili wa kampeni za uchaguzi mkuu kabla ya bunge kuziidhinisha.

Wakiongozwa na mbunge wa Mbeere Kaskazini Charles Njagagua, wabunge hao walidai IEBC ilitaka kulilaumu bunge kwa kukosa kupitisha kanuni hizo, na kuzichapisha bila kufuata utaratibu ufaao.

“Ni wazi kwamba kanuni hizi zinapaswa kuidhinishwa angalau mwaka mmoja kabla ya uchaguzi. Huwezi kuziwasilisha dakika za mwisho, na hata kuzichapisha katika gazeti rasmi la serikali bila idhini ya bunge. IEBC inataka kutulaumu bure,” akafoka Bw Njagagua, ambaye ni naibu mwenyekiti wa kamati ya bunge kuhusu sheria ndogondogo.

Kwa upande wake, Mbunge wa Funyula, Bw Wilberforce Oundo alisema kanuni hizo zilitayarishwa bila umma kushirikishwa, inavyohitajika kikatiba.

“Mambo yanabadilika kila siku. Mkondo wa siasa na matumizi ya pesa miaka minne iliyopita hauwezi kufananishwa na mwaka huu. Kwa hivyo, maoni ya wananchi yalipasa kushirikishwa wakati wa kuandaliwa kwa kanuni hizi zitakazotumika mwaka ujao,” akasema Bw Oundo.

Kauli yake iliungwa mkono na mwenzake wa Gilgil, Martha Wangari aliyesema IEBC kama tume ya kikatiba, haifai kuonekana kuvunja katiba hiyo.

“Tunafahamu kuwa kanuni hizi hazikubadilishwa tangu zilipotayarishwa mnamo 2016. Ikiwa mabadiliko yatafanywa, sharti bunge lihusishwe. Hilo halikufanyika. Kwa hivyo napinga kanuni hizi,” akasema Bi Wangari.

Hata hivyo, IEBC ilijitetea kuwa ilifuata taratibu zote za kisheria kabla ya kuchapisha kanuni hizo.

“Hatukuwa na nia mbaya katika kuchapisha kanuni hizi. Nia yetu haikuwa kulitenga bunge na umma kama inavyodaiwa. Tunahitaji kuomba msaada wa bunge ili kuhakikisha uchaguzi wa mwaka ujao ni huru na wa haki, ” akasema mwenyekiti Wafula Chebukati mbele ya wabunge hao katika majengo ya bunge, Nairobi.

Meneja wa Ufadhili wa Kampeni, Bi Salome Oyugi, aliyeandamana na Bw Chebukati, pia alitetea IEBC akisema kamati yao ilikuwa tayari kuwasilisha sheria hizo bungeni mwaka wa 2017 ili zijadiliwe, ila bunge likaahirisha mchakato huo.

You can share this post!

Malengo yangu ni kushindia PSG taji la kwanza la UEFA...

Duale ajitetea kwa madai alirejelea Kanisa Katoliki kama...