• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Man-United wakomoa Leeds United na kutuma onyo kwa washindani wao wakuu EPL

Man-United wakomoa Leeds United na kutuma onyo kwa washindani wao wakuu EPL

Na MASHIRIKA

MASHETANI wekundu wa Manchester United walituma onyo kali kwa washindani wao wakuu katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) msimu huu kwa kuponda Leeds United 5-1 uwanjani Old Trafford.

Kiungo raia wa Ureno, Bruno Fernandes, 26, alifungia Man-United mabao matatu huku mengine yakipachikwa wavuni na wanasoka Mason Greenwood na Fred de Paula Santos. Leeds walifutiwa machozi na Luke Ayling katika dakika ya 48.

Ilikuwa mara ya kwanza kwa Fernandes kufungia Man-United mabao matatu katika mechi moja tangu atue ugani Old Trafford mnamo Januari 2020.

Aidha, ilikuwa mara ya kwanza kwa mchezaji wa Red Devils kufuma kimiani magoli matatu katika mchuano mmoja wa EPL tangu Robin van Persie afanye hivyo dhidi ya Aston Villa mnamo 2013.

Kati ya masogora wa Man-United walioridhisha zaidi dhidi ya Leeds ni Paul Pogba aliyechangia mabao manne kabla ya kuondolewa uwanjani katika dakika ya 75.

Nafasi ya Mfaransa huyo ambaye pia amewahi kuchezea Juventus ilitwaliwa na sajili mpya Jadon Sancho aliyetua ugani Old Trafford muhula huu kwa Sh11.5 bilioni baada ya kuagana na Borussia Dortmund ya Ujerumani.

Kabla ya kipenga cha kuashiria mwanzo wa mechi hiyo kupulizwa, beki Raphael Varane alitambulishwa kwa mashabiki wa Man-United. Nyota huyo raia wa Ufaransa alisajiliwa kutoka Real Madrid ya Uhispania kwa Sh5.3 bilioni.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Man-United wamtwaa rasmi beki Raphael Varane kutoka Real...

Edwin Ng’ang’a Thuo: Nahodha anayeinua...