• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 8:12 PM
Nitawapa mashine za kisasa kuchapa kazi nikiingia Ikulu 2022, Raila aahidi vijana

Nitawapa mashine za kisasa kuchapa kazi nikiingia Ikulu 2022, Raila aahidi vijana

Na SAMMY WAWERU

DALILI kiongozi wa chama cha ODM Raila Odinga kuwa debeni 2022 kuwania urais zinaendelea kudhihirika.

Awali, Bw Raila amekuwa akikwepa kueleza bayana endapo atashiriki uchaguzi mkuu ujao, akisisitiza kwamba lengo lake kupitia mapatano ya Handisheki kati yake na Rais Uhuru Kenyatta ni kuunganisha taifa.

Amenukuliwa mara kadha akidai atatoa msimamo wake baada ya Ripoti ya Mpango wa Maridhiano (BBI), ila hatma yake kwa sasa ipo mikononi mwa mahakama ya rufaa, kupita.

Kwenye ziara yake eneo la Nakuru kutangamana na vijana Jumanne, Waziri huyu Mkuu wa zamani, aliendelea kumsuta Naibu wa Rais William Ruto kwa sera zake kuinua uchumi kupitia mfumo wa bottom-up.

Akimcharura Dkt Ruto kwa kuwapa vijana wilibaro, Bw Raila alisema endapo ataingia Ikulu mwaka ujao, ataweka mikakati kabambe kuwapa mashine za kisasa kujiendeleza kikazi.

“Sisi tunataka kuona vijana wameinuka. Mazingira yangu nataka yawe ya vijana. Tutaboresha biashara kwa kuwapa mashine za kisasa, wajiendeleze na wengine waweze kuanzisha biashara,” akasema.

“Ninashangaa kuona wengine wakiwapa wilibaro,” Raila akasema akiuza sera zake, matamshi yake yakionekana kulenga Naibu wa Rais Ruto.

Katika ziara yake Nakuru kutangamana na baadhi ya vijana eneo hilo, Raila alikuwa ameandamana na gavana wa kaunti hiyo, Bw Lee Kinyanjui.

Kiongizi huyo wa upinzani na ambaye kwa sasa anashirikiana kwa karibu na Rais Kenyatta baada ya mapatano ya Handisheki, amekuwa akimsuta Dkt Ruto, akitaja ahadi zake kama hadaa tupu, na kwamba angezitekeleza wakati akiwa serikalini kama Naibu wa Rais.

You can share this post!

Mutua na Lilian wafunikia kiini cha kutengana

MAPISHI: Fish cakes