• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 5:46 PM
FAUSTINE NGILA: Usilie ughali wa mafuta, nunua gari la kielektriki

FAUSTINE NGILA: Usilie ughali wa mafuta, nunua gari la kielektriki

NA FAUSTINE NGILA

MAGARI mengi yanayomilikiwa humu nchini na duniani kote yanatumia dizeli au petroli, mafuta ambayo yanachafua mazingira na kutishia maisha ya vizazi vijavyo.

Najua pia kwa wale ambao bado wana ndoto ya kumiliki gari, wanapanga kununua gari linalotumia mafuta kwa kuwa hayo ndiyo magari wanayoona kwenye barabara.

Hawaoni magari ya kielektroniki kwa wingi.Ni kweli kuwa magari ya kielektroniki ni machache, lakini tangu yaingie humu nchini kuanzia 2015, kumekuwa na mjadala muhimu kuhusu iwapo madereva wataendelea kununua mafuta ambayo ni ghali na yanayochafua mazingira au watanunua magari ya kielekntroniki yasiyotoa moshi na yanayohitaji kutiwa chaji kama simu.

Tunaishi katika enzi ambapo mafuta machafu yanaendelea kuchafua anga na kuchangia majanga duniani kama vile mvua kupita kiasi inayosababisha mauti kutokana na mafuriko, mioto ya kila mara kutokana na joto la kiajabu, kuongezeka kwa maji baharini na kuyeyuka kwa theluji milimani kwa kasi isiyowahi kushuhudiwa.

Nimejionea Wakenya wengi wakifurika mitandaoni kuilaani serikali kwa kupandisha bei ya dizeli, petroli na mafuta taa kila mara, lakini wanasahau kuwa mustakabali wa kawi upo kwa vyanzo visivyochafua mazingira kama vile umeme kutokana na miale ya jua, mvuke au upepo.

Ingawa kuna mbinu nyingi za kuhamia kwa magari ya kielektroniki (kielektriki, ukipenda)Kenya yahitaji sera za kudhibiti jinsi magari yanayotumia mafuta yatahifadhiwa au sehemu zake kutumiwa upya, tusije tukajaza taka za kielektroniki tunapoboresha hewa tunayopumua.

Aidha, ni Wakenya wachache tu ambao wanaelewa jinsi injini za magari haya hufanya kazi. Hawajui pia ni wapi kuna vituo vya kuchaji magari ya aina hii. Inamaanisha kuwa hamasisho linahitajika ili wananchi waelewe tija ya ninachozungumzia.

Gharama

Kwa kawaida, gari la kieletroniki litakuondolea gharama ya kununua mafuta. Ni gari ambalo baada ya kuchaji unaweza kuliendesha kwa zaidi ya kilomita 500 ambapo ungetumia mafuta ya Sh5,000. Betri yake nayo hubadilishwa baada ya kati ya miaka minane na kumi.

Hata hivyo, itakuwa safari ndefu kwa Kenya kufikia lengo hili, ikizingatiwa kuwa umeme hata jijini Nairobi hupotea kila mara.

Hali hii sasa inahitaji matumizi ya kawi ya jua ambayo serikali tayari imependekeza sera hasi zinazozuia matumizi yake kule vijijini.

Ni sera hizi ambazo zinafaa kuondolewa ili kuwaruhusu wamiliki wa magari kujenga vituo vya kuchaji magari popote wanapotaka nchini.

Serikali inafaa kupiga jeki mpango huu kwa kujenga vituo vya kuchaji katika barabara zote kuu, na kubuni sera ya kuwataka wamiliki wa vituo vya mafuta kuweka pia mashine za kuchaji magari haya.

Tayari kuna vituo vitatu jijini Nairobi, lakini jinsi dunia imebadilika huenda vituo hivyo vikaongezeka hata zaidi huku mataifa yanayounda magari yakisema kuwa hayatauza magari ya mafuta baada ya mwaka 2030.

Hivyo basi, tunafaa kujiandaa kisaikolojia, kiuchumi na kuweka miundomsingi ifaayo mapema ili kuenda na kasi sawa na mataifa yaliyoendelea.

Iwapo unamiliki gari la mafuta, sasa fahamu kuwa soko la mafuta litaporomoka.Tusipofanya hivi, basi tutakuwa tunachafua mazingira ambayo yanafaa kutumiwa na vizazi vijavyo ambavyo pia vina haki ya kuishi maisha bora.

You can share this post!

WALLAH: Usimtukane mamba kabla hujauvuka mto

Wazee waidhinisha Waiguru awanie ugavana tena 2022