• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 4:25 PM
Rais aongoza Wakenya kuomboleza seneta aliyefariki kwa ajali

Rais aongoza Wakenya kuomboleza seneta aliyefariki kwa ajali

Na Mary Wangari

VIONGOZI na wanasiasa mbalimbali wakiongozwa na Rais Uhuru Kenyatta pamoja na naibu wake, Dkt William Ruto jana waliungana na Wakenya kumwomboleza Seneta Mteule, Victor Prengei, aliyefariki katika ajali ya barabarani.

Kupitia kwa taarifa kwa vyombo vya habari, Rais Uhuru alimtaja marehemu kuwa kiongozi shupavu aliyejitahidi kuboresha maisha ya vijana na jamii za wachache nchini.

“Inahuzunisha sana kuwa kifo kimetupoka kiongozi hodari na mchanga aliyejitahidi kuimarisha maslahi ya vijana na jamii za wachache,” taarifa ikasema.

Seneta huyo wa Chama cha Jubilee aliaga dunia baada ya kuhusika kwenye ajali Jumatatu, saa tatu na robo usiku, kwenye barabara ya Kabarak-Nakuru.

Kulingana na ripoti ya polisi iliyoonwa na Taifa Leo, gari la Bw Prengei lilipoteza mwelekeo katika eneo la Kioto, kabla ya kuyumbayumba na kugonga ukuta.

Seneta huyo aliyekuwa amejeruhiwa alikimbizwa katika Hospitali ya Moi Memorial ambapo alikata roho alipokuwa akitibiwa.

Marehemu alikuwa miongoni mwa maseneta sita waliofikishwa mbele ya Kamati ya Nidhamu katika chama cha Jubilee mapema mwaka huu.Kupitia rambirambi zake, Naibu Rais alimtaja marehemu kama kiongozi aliyejitolea mhanga kutetea haki za walio wachache.

“Taifa letu limempoteza mwanamme muungwana. Seneta Victor Prengei alikuwa mpole na mtumishi wa umma aliyejitolea kuendeleza maslahi ya walio wachache,” alisema.

Huku akifariji familia na jamaa wa marehemu, Kiongozi wa ODM Raila Odinga alimwomboleza Seneta Prengei akisema “kifo chake cha ghafla ni pigo kuu kwa jamii ya Ogiek na bunge.”

Kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka alituma rambirambi zake akisema jamii ya Ogiek, Seneti na taifa kwa jumla limempoteza kiongozi aliyewakilisha matumaini makubwa.

Akielezea kushtshwa na habari hizo, Kiongozi wa Ford Kenya Moses Wetangula alisema Bw Prengei alikuwa muundasheria aliyekuwa na uhusiano mwema na wenzake katika seneti huku akitoa wito kuhusu kuimarisha usalama barabarani.

Kwa upande wake, Seneta Mteule Millicent Omanga alimwomboleza marehemu akisema kuwa juhudi zake zitakumbukwa milele.Seneta wa Nakuru Susan Kihika alimtaja marehemu kama rafiki na “mwakilishi wa vijana mwenye unyenyekevu aliyewakilisha wanajamii walio wachache katika Seneti.”

“Kaka yangu.Hii inaumiza sana. Maisha ni nini hasa? Upo hapa leo kesho umeenda. Mwenyezi Mungu aingilie kati…,” aliomboleza Seneta wa Kericho Aaron Cheruiyot..

You can share this post!

Marufuku ya minisketi UG hatimaye yafutwa

OKA WAKAA NGUMU!