• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 1:29 PM
Linda Katiba wasema waliopendekezwa kuteuliwa makamishna wa IEBC hawafai

Linda Katiba wasema waliopendekezwa kuteuliwa makamishna wa IEBC hawafai

Na CHARLES WASONGA

VUGUVUGU la Linda Katiba limeelezea kutoridhishwa kwake na ufaafu wa watu wanne walioteuliwa na Rais Uhuru Kenyatta kujaza nafasi nne za makamishna wa IEBC.

Wakiongea jijini Nairobi Jumatano, viongozi wa vuguvugu Bw Martha Karua na Dkt David Ndii walisema wanne hao hawakuwa bora zaidi kielimu na kitajriba kusimamia shughuli za uchaguzi.

Francis Wanderi, Justus Abonyo, Juliana Cherera na Irene Cherop waliopendekezwa na Rais Kenyatta Agosti 5, 2021 kujaza nafasi za Dkt Roselyne Akombe, Consolata Nkatha Bocha, Mary Mwanjala na Dkt Paul Kurgat waliojiuzulu mnamo Aprili 18, 2018.

“Inavunja moyo kwamba jopo hilo halikutupatia watu ambao ndio bora zaidi kwa majukumu ya makamishna wa IEBC. Japo huenda wanne hao wamesoma kiasi cha haja, siamini kwamba wana tajriba hitajika kuendesha uchaguzi,” Bi Karua akasema.

Kwa upande wake Dkt Ndii aliwataka wabunge kuhakikisha kuwapiga msasa wanne hao kuhakikisha kuwa wanne hao ni wale ambao wana uzoefu na weledi wa kuendesha uchaguzi.

“Ikiwa hawatakuwa na sifa hizo, basi wabunge wawakatae na nafasi hizo zipewe wengine wengi waliohojiwa na ambao tunaamini wanahitimu kwa kazi hii,” akaeleza Dkt Ndii bila kutaja wale ambao wanawapendelea kwa nyadhifa hizo.

Jopo la uteuzi wa makamanisha wa IEBC chini ya uongozi wa Bi Elizabeth Muli waliwahoji jumla ya watu 36 mwezi jana katika juhudi zake za kusaka watu wanaohitimu kuhudumu kama makamishna wa tume hiyo.

You can share this post!

Mchujo wa UDA utaendeshwa kwa njia huru na haki, Ruto asema

Brentford wasajili kipa Alvaro Fernandez kutoka Uhispania