• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 7:55 AM
Uhuru asimamisha jaji kazi

Uhuru asimamisha jaji kazi

Na BENSON MATHEKA

RAIS Uhuru Kenyatta amemsimamisha kazi Jaji Muthoni Gathumbi wa Mahakama Kuu kufuatia ushauri wa Tume ya Huduma ya Mahakama (JSC) na kuteua jopo la kuchunguza ufaafu wa jaji huyo kuhudumu.

Rais Kenyatta alisema alichukua hatua hiyo baada ya JSC kumweleza kuwa Jaji Gathumbi hawezi kutekeleza majukumu yake ya jaji ipasavyo.

Kulingana na JSC, Jaji Gathumbi aliyekuwa akihudumu katika kitengo cha kusikiliza kesi za mizozo ya ardhi hana uwezo unaofaa kiakili kutekeleza majukumu yake.

“JSC, baada ya kuchunguza ripoti kadhaa za matibabu, iliridhika sababu za kumuondoa ofisini kutokana na kukosa uwezo wa kutekeleza majukumu ya ofisi zilikuwa zimethibitishwa,” Rais Kenyatta alisema kwenye ilani katika gazeti rasmi la serikali.

Sheria inasema Rais akipata ombi kama hilo kutoka kwa JSC, anafaa kuteua jopo kulichunguza.Jopo hilo litachunguza ombi la kumuondoa Jaji Gathumbi ofisini na kuwasilisha ripoti kwa rais.

Jopo hilo litasimamiwa na Jaji Hellen Amolo na wanachama wake ni Majaji Luka Kimaru, na Linnet Ndolo, Bw Peter Murage, Bi Martha Nyakado, Dkt Frank Njenga na Dkt Margaret Othieno.

Ripoti ya jopo hili itaamua iwapo Rais Kenyatta atakubali ombi la JSC la kumuondoa ofisini Jaji Gathumbi.

Hii ni mara ya kwanza kwa JSC kupendekeza jaji kuondolewa ofisini kwa madai inayochunguza. Rais huwa anakubali ombi la tume jopo analoteua linapochunguza na kuthibitisha madai.

Jopo likikosa kuthibitisha madai jaji husika huwa anaendelea kuhudumu.

You can share this post!

Mamilioni yapotelea kwenye miradi duni

Polisi wasaka mshukiwa wa ugaidi aliyekwepa mtego wao