• Nairobi
  • Last Updated April 23rd, 2024 10:10 AM
Wito viongozi wa Mlima Kenya wajipange wawe pamoja kisauti

Wito viongozi wa Mlima Kenya wajipange wawe pamoja kisauti

Na LAWRENCE ONGARO

VIONGOZI wa Mlima Kenya wamehimizwa kuwa na mwelekeo mmoja wakati huu Kenya inapoelekea kuandaa uchaguzi wa mwaka wa 2022.

Mbunge wa Thika Bw Patrick ‘Jungle’ Wainaina, alisema vyama vya kisiasa havistahili kuvunjwa ili kuingia kwa chama kingine.

“Kila chama kina mwelekeo wake kwa sababu ndicho kitakachotumika kutafuta vyeo vya uongozi,” alifafanua Bw Wainaina.

Alitoa wito kwa wananchi popote walipo wawe makini sana wanapowachagua viongozi.

“Ni vyema kuwachagua viongozi wenye maono ambao hawatajihusisha na siasa za migawanyiko. Cha muhimu ni kuwajali wananchi,” alisema mbunge huyo.

Alisema viongozi watakaochaguliwa wakati huu wanastahili kuweka nguvu zao kwa kubuni ajira kwa vijana.

Alisema hata ingawa viongozi wengi wanaangazia kuwania viti vya uongozi, ni sharti pia wawe na ajenda maalum ya namna ya kuwasaidia vijana.

Wananchi pia walihimizwa kutathmini tabia za kiongozi anayewania kiti chochote cha uongozi.

“Wananchi hawafai kuchagua viongozi kutokana na msisimko. Ni sharti maswala kadha ya kimaadili yazingatiwe,” alisema Bw Wainaina.

Aliongeza kuwa asilimia kubwa ya watu wasio na ajira ni vijana na kwa hivyo ajenda muhimu kwa kiongozi yeyote ni jinsi ya kubuni ajira kwa vijana.

Aliyasema hayo alipohutubia waandishi wa habari mjini Thika akiwaeleza maoni yake.

Bw Wainaina ambaye tayari ametangaza azma yake ya kuwania kiti cha ugavana Kaunti ya Kiambu, mwaka ujao wa 2022, alisema ajenda yake kuu itakuwa kubuni ajira kwa vijana.

“Kwanza ningependekeza vijana wajipange kwa vikundi ili waweze kupewa mikopo itakayowapa mwelekeo wa kujisimamia kibiashara. Hiyo ni njia moja ya kujiajiri wenyewe,” alifafanua mbunge huyo.

Alisema mpango huo utafanikiwa iwapo kutakuwa na ushirikiano mwema na wafanyikazi na kuwepo na mazingira mazuri ya kufanya kazi.

You can share this post!

AKILIMALI: Kuku wa kienyeji wanampa donge nono

Okutoyi atinga nusu-fainali ya tenisi ya J3 nchini Misri