• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 9:50 AM
Serikali kutumia vijana na wanabodaboda kuendesha kampeni ya amani kuelekea 2022

Serikali kutumia vijana na wanabodaboda kuendesha kampeni ya amani kuelekea 2022

Na CHARLES WASONGA

SERIKALI itatumia makundi ya vijana na waendeshaji bodaboda kuendesha mipango ya kudhibiti ghasia zinazohusiana na uchaguzi katika maeneo mbalimbali nchini kuelekea uchaguzi mkuu wa Agosti 9, 2022.

Waziri wa Usalama wa Ndani Fred Matiang’i, Jumatano alisema wanachama wa makundi haya mawili watakodiwa kushiriki katika mipango ya kuhubiri amani na kutoa elimu ya uraia.

“Makundi hayo ya vijana na wanabodaboda watashirikiana na mashirika ya kidini na wadau wengine kuendesha shughuli hizo kuanzia ngazi za vijijini hadi mijini,” Dkt Matiang’i akaeleza huku akitoa hakikisho kuwa serikali itadhibiti usalama kote nchini katika kipindi hicho cha uchaguzi.

Waziri alisema kampeni hiyo ya kuhubiri amani italenga maeneo ambayo yametambuliwa kuwa katika hatari ya kushuhudia machafuko na maeneo mengine ambako utafiti wa kiusalama unaendeshwa.

“Sisi katika sekta ya usalama, huwa hatuendeshi chaguzi, tunaandaa mazingira kwa IEBC kuendesha shughuli hizo. Sharti tuhakikishe kuwa uchaguzi unafanywa kwa usalama sawa na upokezaji wa kimamlaka. Tumejitolea kuhakikisha kuwa hakuna risasi itakayofyatuliwa na hakuna raia atakayejeruhiwa; Wakenya wote watasaidiwa kushiriki katika mpango wa kuunda uongozi na demokraasia ya nchi yetu,” Dkt Matiang’i akaongeza.

Waziri huyo alisema hayo katika Kongamano la 64 la Baraza Kuu la Baraza la Kitaifa la Makanisa Nchini (NCCK) lililofanyika katika Ukumbi wa Mikutano ya Limuru, Kaunti ya Kiambu.

Dkt Matiang’i aliongeza kuwa washirika wa kimaendeleo pia watahimizwa kufadhili kampeni za vijana kuhubiri amani nchini “ili kuzima kabisa kero ya fujo ambazo hugubika chaguzi nchini kila mara.”

Waziri ambaye alikuwa ameandamana na mawaziri wasaidizi Mercy Mwangangi (Afya), David Osiany (Biashara) na Zack Kinuthia (Michezo) alitoa changamoto kwa vijana kujisajili kwa wingi kuwa wapigakura ili wawanie nyadhifa za uongozi katika uchaguzi ujao.

You can share this post!

Okutoyi atinga nusu-fainali ya tenisi ya J3 nchini Misri

Wakazi wa Thika wajitokeza kwa wingi kupata chanjo ya...