• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 10:55 AM
Agizo wanafunzi waliokosa kujiunga na sekondari wasakwe

Agizo wanafunzi waliokosa kujiunga na sekondari wasakwe

MAUREEN ONGALA na STANLEY NGOTHO

MAELFU ya wanafunzi hawajajiunga na Kidato cha Kwanza katika kaunti mbalimbali nchini, wiki nne tangu wenzao kuripoti.

Katika Kaunti ya Kilifi, Kamishna wa Ukanda wa Pwani, John Elung’ata, alisema kuwa wanafunzi 12,000 hawajajiunga na Kidato cha Kwanza.

Bw Elung’ata alitoa amri kwa machifu na naibu wao kaunti hiyo kuhakikisha kuwa kila mwanafunzi amejiunga na kidato cha kwanza kabla ya mwezi wa Oktoba.

Bw Elung’ata aliwaomba wasimamizi husika kuwasaka watoto wote ambao hawajaweza kujiunga na Kidato cha Kwanza kutokana na sababu mbalimbali ili wasaidiwe.

Akizungumza na wadau katika shule ya sekondari ya wasichana ya Wakala, Kaunti ndogo ya Magarini, Bw Elung’ata alisema wasimamizi wahusika wanafaa kusimama kidete kuhusiana na masuala ya masomo.

“Machifu wanafaa kuisaidia wizara ya Elimu kutimiza lengo lake la kuhakikisha kuwa kila mtahiniwa wa KCPE amejiunga na sekondari,” akasema Bw Elung’ata.

Aliwahimiza machifu kuhakikisha kuwa watoto wote wanajiunga na kidato cha kwanza bila kujali hali ya kiuchumi ya wazazi wao.Hata hivyo, kamishna wa Kaunti ya Kilifi alisema kuwa tayari machifu wameanza kutimiza jukumu lao.

“Tunaamini ifikapo wiki ijayo, idadi ya watahiniwa watakaojiunga na sekondari itapanda kutoka asilimia 64 hadi asilimia 80,” akasema Bw Olaka.

Katika Kaunti ya Kajiado, zaidi ya wanafunzi 4,000 hawajaripoti katika shule za sekondari.

Wizara ya Elimu katika Kaunti ya Kajiado ilisema kati ya watahiniwa 21,000 waliofanya Mtihani wa Darasa la Nane (KCPE) ni 17,000 pekee waliojiunga na shule za sekondari.

Mkurugenzi wa Elimu wa Kaunti hiyo Luka Kangogo, alisema huenda wazazi walikosa kupeleka watoto wao shuleni kutokana na hali ngumu ya kiuchumi na hatua ya machifu kulegeza kamba.

You can share this post!

Kaunti 4 eneo la Magharibi kupata chanjo mpya

TSC yapata ngao kuzuia walimu kujihusisha na ubodaboda