Na GEOFFREY ANENE
KABRAS Sugar imepiga Strathmore Leos 36-19 nayo KCB ikalima Menengai Oilers 35-17 katika mechi za nusu-fainali za Ligi Kuu ya raga ya wachezaji 15 kila upande maarufu Kenya Cup mnamo Agosti 28.
Wanasukari wa Kabras na wanabenki wa KCB sasa watapepetana Septemba 4 kuamua mshindi wa ligi hiyo ya klabu 11. Mabingwa wa mwaka 2016 Kabras walilemea wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Strathmore kupitia kwa miguso ya Derrick Ashiundu (mitatu) na Jone Kubu na Ntabeni Dukisa (mguso mmoja kila mmoja). Dukisa pia alichangia mikwaju mitatu na penalti mbili katika mchuano huo.
KCB ilipata alama kupitia kwa Jacob Ojee (miguso mitatu), Michael Wanjala (mguso mmoja), Darwin Mukidza (penalti mbili na mikwaju mitatu), na Shaaban Ahmed (mkwaju mmoja).
Kitakuwa kivumbi kati ya Kabras na mabingwa watetezi KCB. Kabras wamewahi kupiga KCB mara mbili pekee tangu waingie Kenya Cup kwa mara ya kwanza kabisa msimu 2014-2015.
Wanasukari wa Kabras, ambao wanatiwa makali na Dominique Habimana, walichapa KCB 19-3 msimu uliopita wa 2019-2020 na kuandikisha ushindi wa pili mfululizo waliponyuka vijana wa kocha Curtis Olago 30-23 zaidi ya wiki tatu zilizopita (Agosti 5). Kabla ya hapo, mabingwa mara saba KCB waligawa dozi kali kwa Kabras.
Takwimu za Kenya Cup za ana kwa ana za nusu-fainali 2021:
Kabras na Strathmore Leos
Kabras 33-19 Strathmore Leos
Strathmore Leos 9-35 Kabras
Kabras 54-7 Strathmore Leos
Strathmore 13-62 Kabras
Kabras 43-13 Strathmore Leos
Kabras 44-13 Strathmore Leos
KCB na Menengai Oilers
KCB 35-17 Menengai Oilers
Menengai Oilers 19-22 KCB
Menengai Oilers 13-43 KCB
KCB 43-13 Menengai Oilers
Menengai Oilers 20-29 KCB
KCB 27-3 Menengai Oilers