• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 8:12 PM
CHOCHEO: Ukitunzwa, jitunze!

CHOCHEO: Ukitunzwa, jitunze!

Na BENSON MATHEKA

VISA vya watu kumezea mate wachumba wa watu vimeongezeka na wakati mwingine kuzua maafa.

Pia imekuwa kama jambo la kawaida walio katika ndoa kuwa na mipango ya kando bila kujali athari zake.

Wanaume waliooa wamekuwa wakiweka vimada, wanawake nao wakiwa na masponsa.

Baadhi ya wanaohusika na michepuko hii wanadai hawaridhishwi na wenzao.

Wataalamu wa masuala ya mahusiano wanasema kwamba tabia hii inayotishia maisha ya ndoa inaweza kuepukwa.

“Tiba ya michepuko ni moja tu. Mume kuheshimu mkewe na mke kuheshimu mumewe. Mke kutunza mumewe na mumewe kutunza mkewe. Hakuna kitu hatari kwa ndoa kama kupuuza mtu wako kwa hali yoyote ile,” asema mtaalamu wa masuala ya mapenzi Samuel Femi.

“Ukitunza mkeo au mumeo apendeze, hautaona urembo wa mwingine. Ukitunza mumeo, hatavutiwa na mwanamke mwingine. Nawe ukitunzwa na mtu wako, elewa anafanya hivyo kwa sababu yake na sio ya watu wengine,” aeleza Femi.

Mtaalamu huyu anasema baadhi ya watu hukosea kwa kuanza michepuko wanapotunzwa na wachumba wao.

“Ni uchungu kuona mtu ambaye umejitolea kwa hali na mali kumtunza apendeze, awe mwanamume au mwanamke, akikusaliti na kuanza kuchangamkia wengine. Hili sio jambo geni, limekuwa likitendeka na linaendelea kutendeka lakini matokeo yake ni balaa na hasara,” aeleza Femi.

Kulingana na Bestella Auma, mwanasaikolojia wa shirika la Tella Counselling Services, hakuna shubiri kali kama mwanamke kugundua kwamba mwanamume aliyetumia muda na rasilmali kumtunza anamezea mate mwanamke mwingine.

“Mwanamke hawezi kuvumilia ushindani kutoka kwa mwanamke mwenzake. Huwa anahisi amedharauliwa, kudunishwa na kutumiwa vibaya,” asema.

Auma anasema uhusiano wa kimapenzi huwa unanawiri wachumba wakishirikiana kama kundi.

“Mume na mke wanaofanya maamuzi pamoja kwa lengo la kushinda huwa wanapata matokeo mazuri yanayojenga uhusiano wao. Katika hali hii, heshima ya dhati ndiyo nguzo,” aeleza.

Anashauri wanaume kubaini kuwa wanawake wa nje wanaowamezea mate, huvutia kwa sababu kuna mtu anayechangia wawe hivyo, au wamewekeza katika maslahi yao.

“Ukiona vimeelea, jua vimeundwa au mtu amejinyima kitu katika juhudi za kutaka avutie. Nyasi inayowekwa maji huwa ya kijani kibichi kila wakati. Vilevile, wekeza katika urembo wa mtu wako kila wakati. Kila mwanamume anaweza kutamani mwanamke mrembo, lakini inachukua mwanamume kamili kufanya mwanamke kuvutia na kuwa mrembo,” aeleza Auma.

Femi anasema wanawake walio katika ndoa wanaomezea mate wanaume wengine wanafaa kusaidia waume zao waweze kufanikiwa maishani.

“Kufaulu kwa ndoa hakuhitaji kuwa na nyumba kubwa ya kifahari au gari kubwa jinsi baadhi ya wanawake wanaochepuka wanavyodhani. Unaweza kupata hivi vyote uwe na raha na ukose furaha. Ukisimama na mtu wako na umsaidie kujikuza, uhakikishe yuko nadhifu, kuwe na uwazi na uaminifu kati yenu, basi mtakuwa sawa,” asema.

Auma ambaye pia ni mhubiri anashauri watu kuwaombea wachumba wao kila siku ili kushinda majaribu ya kushiriki michepuko.

“Ulimwengu umeharibika na majaribu ni mengi. Usisubiri jambo mbaya litendeke ndio uombee mtu wako. Usisubiri hadi mtu wako atumbukie kwenye majaribu. Mkinge kwa maombi,” aeleza.

Femi anakubali kuwa maombi, hasa wachumba wakishiriki sala pamoja, wanaweza kuepuka majaribu mengi ukiwemo mchepuko.

“Kinachofanya watu kuzama kwenye mipango ya kando ni ushawishi kutokana na hali na watu wanaojumuika nao. Chagua marafiki wako vyema. Mtu mmoja hawezi kujenga uhusiano mwenzake akiuharibu. Mapenzi hunawiri pale mume na mke wanashirikiana na sio kuchangamkia mipango ya kando iliyowavuta kando,” asema Femi.

You can share this post!

FUNGUKA: ‘Uungwana achia wazee wa kanisa’

UMBEA: Wakati mwingine mbaya wako ni wewe mwenyewe!