• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 7:55 PM
JAMVI: Ruto kukabiliwa na mtihani mkali 2022 bila ya miungano

JAMVI: Ruto kukabiliwa na mtihani mkali 2022 bila ya miungano

Na WANDERI KAMAU

“NI kinaya kuwa Bw Mwangi Kiunjuri na Bw Moses Kuria ndio wanaoongoza harakati za kushinikiza muungano wa kisiasa katika Mlima Kenya ilhali walikuwa katika mstari wa mbele kumpigia debe Dkt Ruto kuhusu azma yake ya urais 2022. Hili ni dhihirisho la uwepo wa vita baridi vya kisiasa miongoni mwa washirika wa Ruto,” asema Bw Mwangi Waithaka, ambaye ni mdadisi wa siasa.

Wadadisi pia wanaeleza kuwa, ingawa Dkt Ruto analenga kukita siasa zake katika jukwaa la ‘kuondoa ukabila’, huenda hilo likawa gumu, ukizingatia kwamba siasa za Kenya zimejikita katika ukabila.

“Ingawa kuna kizazi tofauti ambacho kimeanza kukita mitazamo ya kisiasa tofauti na ukabila, ni vigumu kwa kiongozi yeyote kuendeleza mikakati ya kujipigia debe bila kuzingatia uhalisia wa kikabila,” asema Bw Samuel Njung’e, ambaye ni mdadisi wa siasa.

Bw Njung’e anasema kuwa hata ikiwa mbinu hiyo ilifaulu mnamo 2017, wakati vyama 14 viliungana ili kubuni Chama cha Jubilee (JP), mazingira ya kisiasa ni tofauti sana wakati huu.

“Kati ya 2013 na 2017, Rais Uhuru Kenyatta na Dkt Ruto walionekana kufanikiwa kuiunganisha nchi. Hakukuwa na migawanyiko na taharuki ya kisiasa kama ilivyo sasa. Uthabiti huo ndio uliwasaidia kuifanya Jubilee kuibuka maarufu na kushinda viti hata katika ngome za uliokuwa muungano wa NASA,” akasema.

Wadadisi wanaeleza kuwa tatizo jingine linalomwandama Dkt Ruto ni ‘laana’ ya kung’ang’aniwa kwa tiketi ya UDA miongoni mwa wagombeaji watakaowania nyadhifa mbalimbali za kisiasa.

Wanasema tatizo hilo ndilo liliandama Jubilee, kiasi kwamba ilikilazimu chama kuandaa duru ya pili ya uchaguzi wa mchujo.

“Ukosefu wa chama kingine utajenga taswira iliyoshuhudiwa 2017, ambapo wawaniaji wengi waliachwa nje baada ya kushindwa kupata tiketi ya Jubilee kuwania nyadhifa hizo. Hali hiyo ni miongoni mwa viini vikuu vya mvutano unaoshuhudiwa kwa sasa katika chama cha UDA,” asema Bw Oscar Plato ambaye ni mdadisi wa siasa.

You can share this post!

‘Malenga Msafiri’ ni dereva wa masafa marefu ila...

JAMVI: Oparanya upanga wa kuifyeka mizizi ya OKA Magharibi