• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 7:55 PM
Chama kipya Pwani kinavyotishia Ruto na Raila

Chama kipya Pwani kinavyotishia Ruto na Raila

Na MAUREEN ONGALA

MIPANGO ya kuzindua chama kipya Pwani kabla uchaguzi ujao ufike, imeshika kasi na kutishia kugeuza mawimbi ya kisiasa katika ukanda huo.

Chama hicho cha Pamoja African Alliance (PAA) kinahusishwa na Gavana wa Kilifi, Bw Amason Kingi na wandani wake ambao husema ukanda wa Pwani unastahili kuwa na chama kikubwa kinachotambulika kitaifa.

Duru ziliambia Taifa Leo kwamba, chama hicho ambacho kilikabidhiwa cheti cha muda cha usajili hivi majuzi kinaendelea kujenga afisi zake katika kaunti mbalimbali kinapojiandaa kusajili wanachama.

Mojawapo ya afisi hizo iko katika Kaunti ya Kilifi, ambayo inatarajiwa kuwa makao makuu yake.Chama cha PAA kitatambuliwa kwa rangi za samawati na manjano, huku nembo yake ikiwa nyumba ya kitamaduni ya Kiafrika.

Kulingana na Bw Kingi, rangi ya samawati ilichaguliwa ili kuashiria thamani ya bahari ambayo ni kitegauchumi kikubwa kinachoweza kukomboa ukanda huo ikiwa rasilimali zake zinathaminiwa na kutumiwa inavyostahili.

“Wakati umefika sasa watu waanze kuzoea rangi ya samawati.Hiyo rangi itatenda maajabu hivi karibuni. Jamii inahitaji nyumba, lakini hatuwezi kuwa tukiita watu waungane ilhali wakati huo huo tunaunga mkono vyama vingine,” akasema Bw Kingi.

Uzinduzi wa chama hicho huenda ukawalazimu Kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga, na Naibu Rais, Dkt William Ruto, kupanga upya mikakati yao wakitaka kupata umaarufu Pwani kabla uchaguzi ujao ufanywe.

Dkt Ruto ambaye anatarajiwa kuwania urais kupitia Chama cha United Democratic Alliance (UDA), amefanya ziara nyingi Kilifi tangu wakati alipofanikiwa kuwavutia upande wake wabunge walioasi ODM wakiongozwa na Mbunge wa Malindi, Bi Aisha Jumwa.

Kwa upande mwingine, imebainika baadhi ya wanasiasa waliobaki katika ODM wanasubiri chama kipya kizinduliwe ili wajiunge nacho.

Hivi majuzi, Bw Kingi alipokonywa wadhifa wake wa uenyekiti katika ODM kwa kushikilia msimamo wake wa kutaka kuwe na chama kipya kikuu cha Pwani, wazo ambalo limekuwa likipingwa vikali na Bw Odinga.

Gavana huyo pia alikataa miito ya baadhi ya wanasiasa waliomtaka ajiunge na Dkt Ruto ndani ya UDA, akisema njia pekee ya Pwani kujikomboa kutokana na changamoto ambazo zimedumu kwa karne nyingi ni kupitia kwa chama kilicho na mizizi ukanda huo ambacho kitatambulika kitaifa.

Aliwataka wanasiasa wa Pwani wanaofululiza kuingia UDA wajifunze kutoka kwa wenzao wa eneo la Kati ambao wameshikilia msimamo kuwa watashirikiana na viongozi wengine wakiwa ndani ya vyama vyao wenyewe.

“Mkishaapishwa kuwa wabunge na maseneta, mtapitia yale yale ambayo mliyapitia katika ODM kwa sababu chama ni cha wenyewe. Naibu Rais hakunihusisha alipokuwa anaunda UDA, lakini ananialika nijiunge na chama hicho,” alionya.

“Mimi nitakuwa mgeni nikienda huko na baada ya siku tatu sitafurahia kuwa huko ndani. Ikiwa watu wengi wanaomuunga mkono Naibu Rais wameonelea heri wafanye hivyo wakiwa katika vyama vyao, mbona eneo la Pwani liwe tofauti? Tunahitaji chama ambacho kitatetea kikamilifu masilahi ya eneo hili. Hatutaki kutishwatishwa tena,” akasema.

Hata hivyo, alisema wakati haujafika kwa Pwani kusimamisha mgombeaji urais hadi wakati viongozi watakapokuwa na umoja.

“Wapwani wangapi wamewahi kuwania urais lakini wakapata chini ya kura 200? Nakubaliana na wale wanaotaka tujitose katika siasa za kitaifa lakini tujengeni boma letu kwanza,” akasema.

Uamuzi wa kuunda chama kipya ulifanywa baada ya juhudi za kuunganisha vyama vitano vilivyo na mizizi Pwani kugonga mwamba.

Viongozi wa vyama vya Shirikisho, Kadu-Asili, Republican Congress, Communist na Umoja Summit wangali wanasubiriwa kutoa mwelekeo kwa wanachama wao.

You can share this post!

Dereva atozwa faini ya Sh70000 kwa kumuua mwanafunzi

Supkem yashutumu serikali kwa mauaji