• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 7:55 AM
Ruto na Kalonzo kumenyana tena Ukambani

Ruto na Kalonzo kumenyana tena Ukambani

Na Pius Maundu

NAIBU Rais William Ruto anatarajiwa kumenyana tena kisiasa na kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka, kwenye uchaguzi mdogo wa wadi ya Nguu/Masumba, Kaunti ya Makueni.

Hili ni baada ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kuwaidhinisha wawaniaji wa vyama vya UDA na Wiper kugombea nafasi hiyo.

Bw Eshio Mwaiwa anawania kwa tiketi ya Wiper huku Bw Daniel Musau akipigania kiti hicho kwa tiketi ya UDA.Hapo jana, wawili hao waliimarisha kampeni zao katika sehemu tofauti kwenye wadi hiyo.

Hata hivyo, waliendelea na juhudi zao huku Bw Timothy Maneno akiapa kurejea kwenye kinyang’anyiro hicho, baada ya kukosa kuidhinishwa na IEBC kuwania.

Alhamisi, tume ilikosa kumwidhinisha, ikitaja hitilafu kwenye stakabadhi zake.Kiti hicho kiliachwa wazi mnamo Juni kufuatia kifo diwani Harris Ngui kwenye ajali ya barabarani.

Kampeni za nafasi hiyo zinafanyika huku serikali ikiendelea kutekeleza kanuni za kudhibiti maambukizi ya virusi vya corona.

Jana, wawaniaji hao wawili na wafuasi wao walihudhuria ibada za maombi katika makanisa kadhaa katika wadi hiyo.

Bw Musau aliipigia debe UDA, akikitaja kuwa chama kinachokubalika na Wakenya kutokana na ushindi ambao kimepata kwenye chaguzi ndogo kadhaa ambazo zimefanyika katika sehemu tofauti nchini kwa miezi michache iliyopita.

You can share this post!

Ruto asema kamwe hatajiuzulu

Kenya yazidi kuteleza Olimpiki za Walemavu