• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 6:55 PM
LEONARD ONYANGO: Wakuu wa shule waliotafuna mabilioni wachukuliwe hatua

LEONARD ONYANGO: Wakuu wa shule waliotafuna mabilioni wachukuliwe hatua

Na LEONARD ONYANGO

HATUA ya wizara ya Elimu kuanzisha mchakato wa ‘kurejesha’ kimya kimya mabilioni ya fedha zilizotumwa kwa wanafunzi na shule hewa kati ya 2008 na 2018, inafaa kushutumiwa vikali.

Katibu wa wizara ya Elimu Julius Jwan, wiki iliyopita alipofika mbele ya Kamati ya Bunge kuhusu Uhasibu (PCA), alikiri kwamba wizara ya Elimu ilituma mabilioni ya fedha kwa wanafunzi na shule zisizokuwepo.

Dkt Jwan alisema hali hiyo ilisababishwa na hatua ya wakuu wa shule pamoja na wakurugenzi wa elimu kutoa taarifa za kupotosha kuhusu idadi ya wanafunzi ili kujipatia fedha za wizi.

Ripoti ya Mkaguzi wa Hesabu za Serikali iliyotolewa miezi mitatu iliyopita ilifichua kuwa wizara ya Elimu ilituma zaidi ya Sh3.7 bilioni kwa wanafunzi na shule hewa katika miaka ya fedha ya 2017/2018 na 2018/2019.Wakuu waliongeza idadi ya wanafunzi ili kujipatia fedha za bwerere.

Ripoti za kupotosha kutoka kwa wakuu hao wa shule ziliidhinishwa na wakurugenzi wa elimu wa kaunti kabla ya kutumwa kwa wizara ya Elimu.Shule ya zaidi ya 2,600 zilinufaika na fedha hizo za bwerere ambazo ziliishia katika mifuko ya wasimamizi wa shule.

Jumla ya Sh105.9 milioni za bwerere zilitumwa kwa wanafunzi hewa katika shule 331 za sekondari za umma katika mwaka wa fedha wa 2018/2019.Ripoti ya Mkaguzi wa Hesabu za Serikali ilionyesha kuwa Sh369 milioni zaidi zilitolewa kwa shule 99 za msingi katika kaunti 13 mwaka huo.

Dkt Jwan aliambia Kamati ya PCA kwamba, wizara ya Elimu imefanikiwa kurejesha jumla ya Sh21.1 milioni tangu 2019.

Mfumo wa NEMIS

Kulingana na Dkt Jwan, ilikuwa vigumu kwa wizara ya Elimu kuthibitisha idadi ya wanafunzi shuleni kwani wakati huo hakukuwa na Mfumo wa Kielektroniki wa Usimamizi wa Elimu (Nemis) unaotumiwa sasa.

Katibu huyo wa Wizara alimbia wabunge kwamba shule zilizopokea fedha za ziada zimekuwa zikikatwa kutoka katika mgao wao.Kupunguza mgao wa shule hizo zilizotumiwa fedha za ziada kunamaanisha kwamba wanafunzi ndio wanaumia.

Haifai kwa wizara ya Elimu kuadhibu wanafunzi ilhali waliohusika na ujanja huo ni wasimamizi wa shule na wakurugenzi wa elimu.

Wakuu wa shule walioongeza idadi ya wanafunzi ili kujipatia fedha za ziada kwa maslahi yao ya kibinafsi wanapaswa kukamatwa na kufikishwa kortini.

Wakurugenzi wa elimu walioidhinisha shule hewa kutumiwa fedha pia hawana budi kuadhibiwa kwa kushindwa kutekeleza wajibu wao na kufanya walipa ushuru kupoteza mabilioni ya fedha.

Wizara ya Elimu inastahili kuripoti uhalifu huo kwa Tume ya Maadili na Kukabili Ufisadi (EACC) na Idara ya Kuchunguza Uhalifu (DCI) badala ya kujaribu kurejesha fedha hizo kimya kimya huku wahusika wakiponda raha na fedha za wizi.

You can share this post!

WANTO WARUI: Mpango wa kulipa walimu wapya mapema ni wazo...

KVF yafanyia timu za taifa za Kenya mabadiliko 11 zikianza...