• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 10:08 PM
Waiguru alia kuhangaishwa tena na EACC

Waiguru alia kuhangaishwa tena na EACC

Na WANDERI KAMAU

GAVANA Anne Waiguru wa Kiringaga amedai kuwa ameanza kuhangaishwa na washindani wake kisiasa baada ya kusema anatathmini mwelekeo wa kisiasa atakaofuata, uchaguzi mkuu wa 2022 unapoendelea kukaribia.

Hapo jana, Bi Waiguru alisema ameagizwa na Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) kufika katika afisi zake, kwa madai ya “matumizi mabaya” ya Sh52 milioni.Kulingana na Bi Waiguru, matumizi ya fedha hizo yaliidhinishwa na Bunge la Kaunti ili kulipa deni ambalo kaunti hiyo imekuwa nalo tangu mwaka 2010.

Alisema deni hilo lilitokana na ugavi wa ardhi ulioendeshwa katika eneo la makazi la South Ngariama, lenye zaidi ya ekari 7,000.

“Ni kinaya kwa EACC kuniagiza nifike katika afisi zake ilhali inafahamu hili ni deni ambalo serikali ya Kaunti imekuwa nalo kwa muda mrefu,” akajitetea gavana huyo kwenye taarifa.Bi Waiguru alihusisha maagizo hayo na “vitisho vya kisiasa” ambavyo amekuwa akipokea tangu Mchakato wa Kubadilisha Katiba (BBI) ulipoanza.

“Harakati za kuipigia debe BBI zilipoanza, nilisema nitatangaza msimamo wangu baada ya muda. EACC ilivamia afisi zangu. Majuzi, nilisema ninatathmini mwelekeo wa kisiasa nitakaofuata, sasa nimepewa maagizo hayo. Je, hii ni sadfa ama ni vitisho ambavyo vimekuwa vikiendeshwa dhidi yangu?” akashangaa.

Hata hivyo, wadadisi wa siasa wanasema kuna uwezekano patashika hizo zinatokana na mwelekeo wa siasa za 2022 katika eneo hilo.

Ingawa Bi Waiguru ametangaza atatetea kiti chake cha ugavana, amekuwa akionekana kuwa miongoni mwa viongozi walio na nafasi kubwa kumrithi Rais Uhuru Kenyatta kama msemaji wa Mlima Kenya.

Baadhi ya viongozi ambao wametangaza nia ya kuwania ugavana katika kaunti hiyo ni Katibu wa Wizara ya Usalama wa Ndani Karanja Kibicho, Mwakilishi wa Wanawake Wangui Ngirichi, kiongozi wa Narc-Kenya Martha Karua kati ya wengine.

Kwa muda sasa, Bi Waiguru amekuwa akimlaumu Dkt Kibicho kwa kutumia ushawishi wake kuingilia utendalazi wa serikali ya kaunti.Hata hivyo, Dkt Kibicho amekuwa akijitenga na madai hayo, akisisitiza yeye ni mtumishi wa serikali na hana azma yoyote ya kujitosa kwenye siasa.

You can share this post!

Joho ajitokeza baada ya muda mrefu, aomboleza kifo cha BBI

Ruto abuni mkakati wa kuangusha Raila Mlima Kenya