• Nairobi
  • Last Updated April 18th, 2024 9:15 PM
Mutua ataka wizara ikomeshe mtindo wa wanafunzi kufika shuleni mapema sana

Mutua ataka wizara ikomeshe mtindo wa wanafunzi kufika shuleni mapema sana

Na SAMMY WAWERU

GAVANA wa Machakos Alfred Mutua amesikitishwa na jinsi wanafunzi hasa wa shule za msingi wanavyolazimishwa kuamka kuelekea shuleni alfajiri na mapema kuliko kawaida. 

Kulingana na Dkt Mutua, hatua hiyo ni kuwapa watoto presha anayohisi Wizara ya Elimu inapaswa kutathmini kwa kina.

“Ninaposafiri kuenda jijini Nairobi, hushangaa sana kuona watoto wakielekea shuleni alfajiri na mapema wengine wakiwa kwenye mabasi,” Dkt Mutua akasema.

Alisema haoni haja ya watoto kushurutishwa kufika shuleni saa hizo, na ambazo alitaja si salama miongoni mwao.

“Ni uerevu upi tunawaongezea kwa kuwalazimisha wawe shuleni kufikia saa kumi na mbili asubuhi?” gavana akataka kujua, akizungumza jijini Nairobi.

Dkt Mutua alisema mfumo wa elimu na masomo ya Kenya unawapa watoto presha na msongo wa mwazo.

“Waziri wa Elimu majuzi alisema watoto wanaweza kuenda shuleni na mavazi ya nyumbani, kwa sababu hizi ni nyakati ngumu. Ni vyema atoe mapendekezo kama hayo na mabadiliko ya saa ambazo watoto wanapaswa kuwa shuleni. Wasiwe wanaenda mapema sana,” Dkt Mutua akasema.

Wizara ya Elimu chini ya Prof George Magoha, inaendelea kutekeleza mfumo mpya wa masomo unaojikita katika umilisi (CBC) na ambao unalenga kuboresha sekta ya elimu nchini.

CBC inapania kufutilia mbali mfumo wa 8-4-4 na ambao umedumu muda mrefu.

You can share this post!

UN yalaani mapinduzi Guinea

Gozi la Brazil dhidi ya Argentina latibuka kwa madai...