• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
TAHARIRI: Polisi wakabiliane na sarakasi za siasa

TAHARIRI: Polisi wakabiliane na sarakasi za siasa

KITENGO CHA UHARIRI

SARAKASI na fujo zilizoshuhudiwa katika Kaunti ya Nyeri jana wakati wa ziara ya Naibu Rais William Ruto hazikustahili.

Dkt Ruto na wafuasi wake walidai kushambuliwa na kurushiwa mawe na watu waliowashuku kuwa wafuasi wa Mbunge wa eneo la Kieni, Kanini Kega.

Baadhi ya wakazi wa Nyeri waliyakana madai hayo, wakisema waliwaona vijana ambao mara kwa mara huandamana na Mbunge wa Mathira, Rigathi Gachagua kwenye misafara yake.

Hatuna namna ya kuyathibitisha madai ya pande zote mbili.

Kwa hivyo, tutajikita zaidi kwenye matukio yenyewe.

Msimu wa siasa, wanasiasa hutumia kila mbinu kuungwa mkono na wapigakura, ikiwemo kuzua fujo au kubuni matukio ya kuwafanya waonewe huruma.

Vyovyote iwavyo, ghasia, fujo au watu kudai eneo fulani ni lao na mwanasiasa wasiyekubaliana naye kifikra hafai kulizuru, ni mambo yanayofaa kukemewa.

Katiba inaruhusu na kukubali Mkenya kuwania uongozi na kuomba kura katika pande zote za nchi, hasa akiwa anawania urais.Dkt Ruto ameshatangaza kwamba atakuwa debeni Agosti 2022.

Kujitokeza katika maeneo ya nchi kuomba kura ni haki yake. Kama kweli waliomrushia mawe walikuwa wa upande wa viongozi wa mrengo wa Kieleweke, basi hayo ni makosa.

Licha ya yeye, hata Kinara wa ODM Raila Odinga, Musalia Mudavadi (ANC), Kalonzo Musyoka (Wiper) na wengine ambao hawajatangaza azma zao, wana haki ya kuzuru Nyeri na kwingineko Kenya.

Lakini pia kama ni kweli viongozi wa mrengo wa Tanga Tanga walibuni tukio hilo ili kujinufaisha kisiasa, basi wakome.

Siasa sawa na dini, huibua hisia kali miongoni mwa wananchi. Mtu kwa kuunga mkono upande mmoja wa siasa, anaweza kusahau ukoo na kutengana na jamaa zake. Huhitaji kuchochewa kidogo tu ili kulipuka.

Kwa hivyo wanasiasa wanapaswa kuwa makini na kuepuka visa vyovyote vya kuibua hisia za wananchi.

Aidha, idara za usalama twazihimiza zichunguze matukio kama ahaya na kuchukua hatua hadharani, ili watu wengine wenye nia ya kusababisha fujo wapate funzo.

You can share this post!

Tuju amtaka Ruto awakanye wandani wake kushambulia familia...

Lukaku afunga bao lake la 67 katika mechi ya 100 ndani ya...