• Nairobi
  • Last Updated April 19th, 2024 8:55 PM
TAHARIRI: Serikali iviondoe vizingiti vya CBC

TAHARIRI: Serikali iviondoe vizingiti vya CBC

KITENGO CHA UHARIRI

SUALA kuhusu mfumo mpya wa elimu (CBC) limejitokeza tena, safari hii hata walioshirika kuubuni wakilalama kuwa unakandamiza wazazi.

CBC ambayo serikali inaipigia debe kuwa njia bora kwa watoto kujitegemea siku za usoni, imekosolewa kuwa inayosababisha usumbufu.

Wazazi wengi wanasema ni kama walioshiriki kuja na fikra za mfumo huo walikuwa wakiwawaza matajiri pekee.

CBC si mfumo wa elimu kwa mtu maskini kama ilivyokuwa 8-4-4.

Tofauti kubwa ni kwamba, wakati wa 8-4-4 watoto walitakiwa kupeleka shuleni vifaa vilivyokuwa viko kwenye nyumba zao.

Mmoja angeagizwa apeleke viatu vya ngozi. Mwenzake angeitishwa rangi ya viatu. Mwengine angeagizwa apeleke taa ya chemni na jivu na kadhalika.

Wanafunzi hao wangefundishwa jinsi ya kusafisha kioo cha taa au kupiga rangi viatu.

Lakini CBC inamchukulia kila mzazi kuwa mwenye uwezo wa kununua bidhaa.

Mwalimu huitisha darasa zima lipeleke mrundo wa vitu.

Gharama nyingine ipo kwenye vitabu.

Ingawa vitabu vya CBC bei yake ni ya wastani, kila mzazi hutakiwa kununua angalau vitabu kumi na kimoja.

Hata somo la mazoezi ya viungo (PE) limeandikiwa kitabu.

Katika mfumo wa sasa, mbali na vitabu wazazi huitishwa vitu vingi. Kuna udongo wa kununuliwa madukani, kuna makasi, nyuzi na vitu vingine vingi.

Walimu bila kujali hali ya kifedha ya wazazi, hutaka vifaa vyote vipatikane kwa wakati mmoja.

Mtu yeyote anayeelewa taaluma ya ualimu anatambua kwamba, vifaa vyote haviwezi kutumika kwa pamoja.

Kwenye mpango wa ufundishaji, Mwalimu hufundisha jambo moja kwa kipindi. Iwapo wanafunzi watakuwa hawajaelewa, humbidi arejelee somo hilo au afanye marudio mafupi kabla ya kusonga mbele.

Kuwaitisha wazazi kila siku ni usumbufu unaoweza kuepukwa.

Wizara ya Elimu katika kupanga ratiba ya mihula, imeongeza masaibu kwa wazazi kwa kuwa na mapumziko mafupi.

Mzazi kumtumia mwanawe nauli aende nyumbani wikendi pekee kwa mapumziko kisha arejee shuleni ni gharama isityostahili.

Wakati huu ambapo watu wanakabiliwa na gharama ya masisha kutokamna na Covid-19, ni muhimu kwa wadau kufikiri upya jinsi ya kuondoa usumbufu kwenye mfumo wa CBC.

You can share this post!

Pele afanyiwa upasuaji kuondoa uvimbe wa utumbo

Rais Conde alivyochotwa na makomando wa kijeshi