• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 12:26 PM
WANGARI: Uhifadhi wanyamapori ni turathi kuu kwa vizazi vijavyo

WANGARI: Uhifadhi wanyamapori ni turathi kuu kwa vizazi vijavyo

Na MARY WANGARI

SHIRIKA la Huduma kwa Wanyamapori Nchini (KWS) mapema wiki jana lilitoa ripoti kuhusu idadi ya wanyamapori nchini baada ya shughuli ya kuhesabu iliyochukua muda wa miezi mitatu tangu Mei.

Ripoti hiyo iliashiria matumaini makuu huku idadi ya wanyamapori kadhaa wakiwemo twiga, pundamilia, swara, kifaru na ndovu ikionekana kuongezeka pakubwa.

Aidha, ripoti hiyo ilifichua nyanja zinazohitaji kutiliwa maanani hasa kuhusu wanyama wanaozidi kudidimia na kukabiliwa na tishio la kutoweka kabisa kama vile simba na chui.

Wanyamapori huchangia nafasi muhimu katika uchumi wa taifa kwa kuvutia watalii kutoka humu nchini na kutoka mataifa ya kigeni, wanaoleta fedha za kigeni.

Ripoti ya takwimu kuhusu idadi ya wanyamapori nchini itapiga jeki pakubwa juhudi za uhifadhi wa wanyama hao kwa kuiwezesha serikali kubuni mikakati thabiti kuhusu raslimali hiyo.

Ni vigumu kutenganisha uhifadhi wa wanyamapori na kulinda mazingira kwa jumla hasa ikizingatiwa kwamba mazingira asilia kama vile misitu, nyika ndiyo makao kwa wanyama hawa.

Aidha, wanyamapori hutegemea chemchemi za maji na hewa safi, misitu na vichaka ili kupata lishe na kuendelea kuishi.

Mbali na kuwa kitega uchumi, wanyamapori vilevile ni urithi wetu tuliopata kutoka mababu zetu tangu jadi.

Tangu jadi, babu zetu walifahamu kutangamana na wanyamapori katika mazingira asilia licha ya kuendelea na shughuli zao za kila siku, hata kabla ya mbuga na hifadhi za wanyamapori kuanzishwa.

Kwa mantiki hii, ni bayana kwamba tuna jukumu muhimu la kuwalinda wanyamapori kwa vyovyote vile ili kupokeza vizazi vijavyo fahari hii tunayojivunia kama taifa.

Inatamausha hata hivyo kwamba, kwa muda mrefu, tishio kuu dhidi ya wanyamapori limekuwa binadamu.

Kupitia uwindaji haramu, kuwafurusha wanyamapori kwenye makao yao asilia, binadamu amesalia kero kuu linalohujumu juhudi za kuhifadhi wanyama hawa na raslimali asilia.

Kadri idadi ya binadamu inavyozidi kuongezeka, ndivyo mazingira asilia wanamoishi yanavyozidi kuharibiwa kupitia ukataji wa misitu na vichaka yanayogeuzwa makazi ya binadamu na mashamba ya kilimo.

Maendeleo kimiundomsingi vilevile hayajasitiri wanyamapori ambapo baadhi ya miradi inayoendeshwa na serikali kama vile barabara na reli, inapitia kwenye makao ya wanyama hawa hivyo kuwavuruga katika mazingira yao asilia.

Hatuwezi kupuuza umuhimu wa maendeleo kimiundomsingi katika kizazi hiki.

Hata hivyo, ni sharti mikakati kabambe ibuniwe kutilia maanani mahitaji kimaendeleo katika kizazi hiki na wakati huo vilevile, kuhakikisha uhifadhi wa wanyamapori na mazingira kwa jumla.

Isitoshe, ni muhimu kuwashirikisha wanajamii wanaoishi karibu na wanyamapori ikizingatiwa kwamba asilimia kubwa huishi katika mazingira asilia nje ya mbuga na hifadhi za wanyama.

Uhifadhi wa wanyamapori unahitaji ujumuishaji wa wadau wote husika ikiwemo serikali na wanajamii ili kulinda raslimali hii na kuipokeza kwa vizazi vijavo.

[email protected]

You can share this post!

ODONGO: Kitui, Kibwana, Muturi na Karua wana mtihani

AKILIMALI: Unavyoweza kudumisha rutuba ya udongo kwa...