• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 11:38 AM
TAHARIRI: Ahadi ya kazi kwa vijana iko wapi?

TAHARIRI: Ahadi ya kazi kwa vijana iko wapi?

KITENGO CHA UHARIRI

KISA cha wasomi watatu waliohitimu na shahada ya uzamifu (PHD) kulazimika kufunza shule za chekechea na msingi kwa kukosa kazi katika shule za upili, vyuo vikuu na taasisi husika za serikali kinatamausha na kukatisha tamaa wanafunzi wengi waliofuzu na digrii ya kwanza katika vyuo vikuu nchini.

Dkt John Timon Owenga, Dkt Violet Otieno na Dkt Daughty Akinyi wanasema kwamba wamelazimika kufunza shule za msingi licha ya kubobea katika taaluma zao kwa kuwa hawajafaulu kupata kazi au kupandishwa vyeo.

Licha ya watatu hao kutumia nguvu, muda, pesa na kujitolea kufikia kiwango cha juu zaidi cha elimu Kenya, hawajaweza kupata kazi zinazowiana na elimu yao katika serikali za kaunti, serikali ya kitaifa, vyuo vikuu au mashirika ya serikali. Hii ndio taswira kamili ya watu wengi waliofuzu chuo kikuu humu nchini.

Wengi hawana kazi na wamesalia kufanya vibarua ili kujikimu kimaisha.Juzi, habari za wanachuo watatu wanaofanya kazi timboni wakilipwa Sh100 zimezagaa kote mitandani.

Amos Kimutai, aliyefuzu katika Chuo Kikuu cha Kisii na digrii ya Kemia ya Mafuta alisema kwamba yeye na rafiki zake hutengeza kokoto wakilipwa Sh100 kwa siku kwa sababu hawakupata kazi baada ya kufuzu.

Ni mahafala wangapi wanafanya kazi kama walinzi wa usiku mijini? Ni wangapi ni mayaya? Kuna tatizo kubwa la ukosefu wa kazi nchini, ingawa tatizo hili laweza kutatuliwa kwa juhudi za pamoja.

Mojawapo ya manifesto na ajenda ya serikali ya Jubilee ilikuwa kuunda ajira milioni moja kila mwaka kwa vijana wetu ili kupunguza kiwango cha ukosefu wa kazi miongoni mwao.

Hilo halikutimia, kilnachoshuhudiwa sasa hivi ni malumbano ya kisiasa yanayopandikiza chuki na uhasama miongoni mwa Wakenya badala ya siasa safi zenye kuboresha hali na maisha yao.

Serikali ya Rais Kenyatta imefanya mengi kuhusu miundomsingi, barabara nyingi zimejengwa katika maeneo mengi nchini, mitaani na mashinani.

Juhudi zizo hizo zilihitajika kupiga jeki sekta za kilimo, utalii, teknolojia, elimu na kwa jumla tasnia ya uzalishaji ili kujenga nafasi tele za kazi.

Wanachuo waliofuzu nao pia wanaweza kutumia maarifa waliopata vyuoni kubuni nafasi za kazi badala ya kutegemea serikali kuwaajiri. Elimu ya juu inapaswa kutanua ubongo na maarifa ya mtu ili afikirie zaidi ya kuandikwa kazi.

You can share this post!

35 kupigania fursa ya kucheza dhidi ya Bandari FC

Waiguru adai ni vigumu kuchaguliwa kupitia Jubilee