• Nairobi
  • Last Updated April 24th, 2024 2:08 PM
MATHEKA: Viongozi wasitumie ukame kujikweza kisiasa raia wakiumia

MATHEKA: Viongozi wasitumie ukame kujikweza kisiasa raia wakiumia

Na BENSON MATHEKA

IDARA ya utabiri wa hali ya hewa imetangaza kuwa mvua inayotarajiwa nchini kuanzia Oktoba haitakuwa ya kutosha.

Hii inamaanisha kuwa kutakuwa na kiangazi kitachoathiri mamilioni ya Wakenya. Hali hii ikitokea, idadi ya Wakenya wanaokabiliwa na ukame itaongezeka hadi milioni sita.

Kwa wakati huu, takwimu za serikali na mashirika tofauti zinaonyesha kuwa, watu zaidi ya milioni mbili wanakabiliwa na ukame.

Kulingana na Waziri wa Ugatuzi Eugene Wamalwa, serikali imetenga Sh2 bilioni kukabiliana na ukame unaoendelea katika kaunti 13.

Mashirika ya kutoa misaada yanakadiria kuwa ukame huu utaenea hadi kaunti 23 kufikia Novemba 2021 ikiwa mvua haitanyesha jinsi wataalamu wanavyobashiri.

Hii inaashiria hatari kubwa kwa nchi kwa jumula.

Kwanza, mamilioni ya watu maskini wanakabiliwa na hatari ya kufa njaa na kiu, watoto kuathiriwa na utapia mlo na wengi kuacha masomo.

Mifugo ambao ni tegemeo la wakazi wa kaunti zaidi ya 13 nchini huenda wakaangamia kwa kukosa malisho na maji.

Kuna hatari ya mizozo kati ya wanyama na binadamu ambayo huwa inaongezeka wakati wa kiangazi.

Tayari, kumekuwa na visa vya jamii kupigania maeneo ya maji na malisho ambapo watu wameuawa.

Ingawa ukame ni janga ambalo binadamu hana uwezo wa kulizuia, serikali imekuwa ikichelewa kuchukua hatua kwa wakati unaofaa licha ya wataalamu wa hali ya hewa kutoa onyo mapema kuhusu hatari ya kiangazi au mafuriko.

Lengo la onyo hilo, ambalo huwa linatolewa mapema huwa ni kuwezesha serikali kujipanga kuzuia hasara, jambo ambalo nadra hufanyika.

Kwa kutochukua hatua, visa vya watu kuuawa na njaa na kiu au ghasia za kijamii zinaporipotiwa, serikali huwa imefeli katika jukumu lake la kulinda raia dhidi ya majanga.

Wakati mwingine serikali huonekana kutokuwa na habari watu wakifariki kwa njaa hadi masaibu yao yanapoangaziwa na vyombo vya habari.

Hii ni aibu kwa serikali iliyo na mfumo thabiti wa utawala uliofadhiliwa na pesa za umma.

Huu ukiwa msimu wa siasa za uchaguzi mkuu, wanaohangaika kwa sababu ya kiangazi wanaweza kusahaulika viongozi wakishughulika na mipango ya uchaguzi mkuu ujao.

Kinaya ni kuwa, wanasiasa watatumia mabilioni ya pesa kwa kampeni zao badala ya kusaidia raia wanaokabiliwa na njaa.

Tumeona baadhi ya viongozi wakichanga mamilioni makanisani lakini hatujawaona wakisaidia wanaokufa kwa njaa.

Sio ajabu baadhi yao wataingiza siasa kwenye masaibu ya raia wanaoangamizwa na njaa na kiu.

You can share this post!

‘Ruto alishika Uhuru mateka’

WASONGA: Serikali itatue changamoto zinazokumba mtaala mpya