• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 4:55 PM
WASONGA: Serikali itatue changamoto zinazokumba mtaala mpya

WASONGA: Serikali itatue changamoto zinazokumba mtaala mpya

Na CHARLES WASONGA

SERIKALI inafaa kushughulikia changamoto zinazozonga utakelezaji wa Mtaala mpya wa Umilisi na Utendaji (CBC) ambao ulianza kutekelezwa nchini mnamo 2019 katika shule za msingi.

Katika kipindi cha siku kadhaa zilizopita, wadau katika sekta ya elimu wameangazia changamoto kadhaa zinazokumba utekelezaji wa mtaala huu wakihofia huenda zikavurugu ufanisi wake na mustakabali wa wanafunzi.

Miongoni mwao ni gharama ya vitabu na vifaa vinavyohitajika katika ufundishaji wa masomo yaliyoko chini ya mtaala huu.

Baadhi ya wazazi wanalalamika kuwa, wanahitajika kununua vitabu vingi kiasi kwamba, baadhi yao wanajikuta kutumia Sh10,000 kununua vitabu na vifaa kwa kila mtoto.

Pili, shule nyingi haswa zile za umma hazina mitambo inayohitajika kufanikisha utelekelezaji wa mtaala huu wa CBC, kama vile kompyuta.

Licha ya hayo, walimu huwapa wanafunzi kazi za ziada za kufanyia nyumbani na ambayo inawahitaji kutoa maelezo, picha na michoro kutoka kwa intaneti.

Hali hii imewalazimu baadhi ya wazazi wenye uwezo kifedha kuwanunulia watoto wao tarakilishi.

Wale ambao hawana uwezo kifedha wanalazimika kulipia huduma hizo katika vituo vya huduma za mtandaoni, maarufu kama cyber café.

Katika maeneo ya mashambani, huduma kama hizi hazipatikani kwa haraka, hali inayowaweka wanafunzi na wazazi katika hali ngumu.

Tatu, ni jambo la kusikitisha kuwa miaka mitatu baada ya Wizara ya Elimu kuanza kutekeleza mtaala wa CBC, kuna baadhi ya walimu ambao hawajapokea mafunzo maalumu kuhusu mbinu ya kuufundisha.

Isitoshe, wale ambao wamepokea mafunzo hayo hawajapata uelewa wa kutosha, na hivyo kuchangia kutekeleza CBC kinyume na ilivyotarajiwa.

Mnamo 2019, aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Kitaifa cha Walimu (Knut) Wilson Sossion alipinga kile alichotaja kama kuharakishwa kwa utekelezaji wa CBC.

Bw Sossion, ambaye pia ni Mbunge Maalumu, alilalamika kuwa Wizara ya Elimu ilianzisha utekelezaji huo pasina kufanya mashauriano tosha na wadau, haswa walimu.

Vile vile, alitaka utekelezaji wa mtaala huo uahirishwe ili kutoa nafasi kwa walimu wote kupewa mafunzo, hususan kuhusu namna ya kuzichambua dhana mbalimbali na kuzitekeleza.

Lakini Waziri wa Elimu George Magoha alimpuuzilia mbali Bw Sossion akimwonya dhidi ya “kuingiza siasa katika mpango unaonuia kuwafaidi watoto wa taifa hili.”

Hata hivyo, sasa dosari ambazo Bw Sossion alikuwa akilalamikia zimeanza kujitokeza kufuatia malalamishi kutoka kwa wadau, haswa wazazi.

Ama kwa hakika, Serikali kupitia wizara ya Elimu ilikiuka Katiba ya sasa kwa kutohakikisha mtaala huo mpya umejadiliwa kwa kina na wadau kabla ya utekelezaji wake kuanza.

Endapo maoni na mapendekezo ya wadau yangekusanywa na kujadiliwa kabla ya mtaala huu kutekelezwa, suala kuu la gharama ya utekelezaji huo lingeshughulikiwa mapema na suluhu kupatikana.

Hali ya sasa ambapo wazazi wanahitaji kununua zaidi ya kitabu kimoja cha kiada kwa somo moja, kando na vifaa vinginevyo lingeshughulikiwa.

Lakini kimsingi, mtaala wa CBC ni mzuri ila utekelezaji wake ndio ulifanywa visivyo.

Kwa mfano, masomo yanayofundishwa yanalenga kumfinyanga mwanafunzi ili aweze kujitegemea pindi atakapomaliza masomo. Mfumo huu pia unalenga kubaini uwezo na talanta za wanafunzi mapema kwa ajili ya kuzikuza kwa manufaa yake siku za usoni.

You can share this post!

MATHEKA: Viongozi wasitumie ukame kujikweza kisiasa raia...

Kamket alala seli tena Lempurkel akijitetea