• Nairobi
  • Last Updated April 16th, 2024 6:55 PM
TAHARIRI: Tuwekeze katika soka ya kina dada

TAHARIRI: Tuwekeze katika soka ya kina dada

KITENGO CHA UHARIRI

ILIKUWA shangwe, vigelegele, hoihoi na nderemo pale wasichana wa kikosi cha soka cha Vihiga Queens walipofuzu kwa dimba la Klabu Bingwa Afrika (CAF) ambalo linachezwa kwa mara ya kwanza nchini Misri baadaye mwaka huu.

Mafanikio hayo yalitokana na hatua ya Vihiga kuibuka mabingwa wa kandanda ya Baraza la Shirikisho la Soka ukanda wa Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) iliyotia nanga Alhamisi jijini Nairobi.

Vihiga alichabanga Commercial Bank of Ethiopia mabao 2-1 kwenye fainali kali iliyosakatwa katika uwanja wa Kasarani, Nairobi.

Hakika soka ya Kenya, upande wa kinadada imekuwa ikipanda hadhi katika miaka ya hivi karibuni hasa tangu kikosi cha taifa cha Harambee Starlets kifuzu kushiriki fainali za Kombe la Afrika mnamo 2018, hii ikiwa mara ya kwanza kabisa kwa taifa hili.

Tangu wakati huo, mchezo wa kinadada wa Kenya umekuwa ukistawi aste aste kila mwaka licha ya ligi ya wanawake nchini kukumbwa na misukosuko ya kila aina hasa kutokana na ukosefu wa ufadhili.

Je, iwapo hadhi ya kabumbu ya Kenya imekuwa ikipaa hivyo ilhali hamna ufadhili wa kutosha, sembuse ufadhili huo ukizidishwa?

Waama, sawa na Harambee Starlets, Vihiga Queens wametupa kila sababu ya kuhakikisha kuwa tunamakinikia zaidi mchezo wa vipusa.

Ni wakati muhimu kwa mashirika mbalimbali hasa ya kibiashara kama vile benki, kampuni za mawasiliano, fedha, usafiri na kudhalika kujitokeza kuinua mchezo wa wasichana wetu.

Wala hii haina maana kuwa macho yaondolewe kwa mchezo wa wavulana; la hasha.

Fani hiyo bado pia inahitaji kukuzwa maadamu ina umuhimu mkubwa hasa kwa maisha ya vijana hao wa kiume.Ufadhili huu una umuhimu nomi kwa maisha ya vijana wa taifa hili.

Kwa kuwekeza katika mchezo huu wa soka hasa upande wa vigoli, tutazuia matatizo mengi nchini yanayowakubwa watoto wa jinsia hiyo.

Wataepuka maovu kama vile mapenzi ya kiholela, ndoa za mapema na hata mihadarati kwa kujishughulisha zaidi na mpira.

Mpira wa mguu, kama shughuli ya kuwatafutia vijana ajira, inastahili kuzingatiwa zaidi na serikali pamoja na wadau ili kuhakikisha kuwa pengo kuu la uhaba wa kazi linazibwa.

Mafanikio ya Vihiga Queens yaibue mwamko mpya kwa wadau katika sekta hii mbali na wawekezaji ambao kwa hakika huvuna pesa nyingi kama faida kila mwaka kutokana na mauzo wanayofanya ambayo hufanikishwa na wateja ambao hasa ni raia wa Kenya.

You can share this post!

FUNGUKA: ‘Sitoi hata ndururu’

Kampuni ya pembejeo kuzindua kiwanda cha kutengeneza mbolea...