• Nairobi
  • Last Updated April 20th, 2024 3:03 PM
TAHARIRI: Lalama kuhusu CBC zisipuuzwe

TAHARIRI: Lalama kuhusu CBC zisipuuzwe

KITENGO CHA UHARIRI

MJADALA kuhusu ufaafu na utekelezaji wa Mtaala mpya wa Umilisi na Utendaji (CBC) umedumu kwa muda sasa huku wazazi na walimu wakilalamika.

Waziri wa Elimu, Prof George Magoha amesisitiza kuwa mtaala huo utaendelea kutekelezwa na kwamba serikali imeweka mikakati ya kuufanikisha kikamilifu.

Kulingana na Prof Magoha, wanaolalamika kuhusu mtaala huo wanautakia mabaya usifaulu akisema serikali haina nia ya kuutupilia mbali.

Hata hivyo, malalamishi ya wazazi na wadau wengine si ya kutaka mtaala huo ukomeshwe bali uboreshwe zaidi kwa manufaa ya wanafunzi na wazazi pia.

Wazazi wanahisi kwamba wamelimbikiziwa majukumu mengi ya kuwasaidia wanafunzi wao ilhali kuna baadhi yao ambao japo wana muda, hawana ufahamu wowote kuhusu wanayotakiwa kutekeleza.

Kuna wale ambao hawakusoma ilhali wanatakiwa kusaidia watoto wao kwa kazi za shuleni na kuna wale ambao wamesoma lakini hawana ufahamu wa masuala ya teknolojia ambayo yamepewa umuhimu katika mtaala huo.

Kuna pia gharama ya vitabu na vifaa ambayo waziri alipuuza lakini ni muhimu sana.

Ingawa anasema serikali imenunua vitabu vya kutosha katika shule zote za umma, kuna suala la usawa ambalo linafaa kushughulikiwa.

Hii ni kwa kuwa wanafunzi wote hawawezi kutoshea katika shule za msingi za umma.

Huu ni ukweli ambao hauwezi kupuuzwa. Muhimu kabisa ni mipango ya serikali ya kuhakikisha wanafunzi wa kwanza wa gredi ya sita wataendelea na masomo ya shule ya upili bila kutatizika.

Licha ya walimu kutilia shaka uwezo wa kufanikisha wanafunzi wa gredi ya sita kujiunga na shule za msingi, Prof Magoha anasema wanaolaumu serikali wanafaa kusubiri kuona mikakati ya serikali.

Kauli ya waziri huyo inaashiria kuwa huenda kuna mipango ambayo serikali imekuwa ikifanya bila kuwahusisha walimu ambao inategemea kufanikisha mtaala huo.

Ikiwa huo ndio ukweli, serikali itakuwa imekosea kwa kuwaacha walimu gizani ilhali inawategemea kutekeleza mtaala huo.

Ili kuepuka malalamishi na sintofahamu, uwazi unahitajika kwa kuwa mtaala wa elimu huwa si mali ya watu wachache bali huwa unabuniwa kustawisha nchi.

Mtaala huo unaweza kuboreshwa kwa kusikiliza malalamishi yanayoibuka na kuyajibu au kuyashughulikia kikamilifu na si kwa kuyapuuza.Kwa kufanya hivyo, mtaala huu utafaulu na kunufaisha nchi.

You can share this post!

Kampeni: Wabunge wako mbioni kubatilisha kanuni za IEBC

Fidu aahidi makubwa kwa mashabiki wa Changamwe Ladies