Na SAMMY WAWERU
KAMPUNI ya kutengeneza pembejeo Elgon Kenya imetangaza kwamba itazindua kiwanda cha kuunda mbolea itakayosaidia kuangazia changamoto za udongo.
Huku wakulima wengi wakiendelea kuhangaishwa na udongo wenye asidi kupita kiasi, kampuni hiyo imesema fatalaiza itakayokuwa ikitengeneza itakuwa na madini ya kuurutubisha.
Aidha, mbolea itasheheni virutubisho kuboresha udongo ulioathirika kutokana na kemikali.
Mkurugenzi Mkuu wa Elgon Kenya Ltd, Dkt Bimal Kantaria amesema uzinduzi wa kiwanda hicho utasaidia kuleta afueni hasa kwa wakulima wenye mashamba madogo na yale ya kadri, ambao kwa muda mrefu jitihada zao kuzalisha chakula zimekuwa zikilemazwa na udongo usio na virutubisho vya kutosha.
“Tutawasaidia kufanya vipimo vya udongo, na virutubisho vinavyokosekana tunawaundia fatailaza ya kipekee yenye madini faafu kuviongeza,” Dkt Bimal akasema.
Alisema mbolea itakuwa ikiundwa kulingana na mahitaji ya udongo, baada ya vipimo kufanywa na kubaini virutubisho vinavyokosa.
Kiwanda hicho kitatumia mashine za kisasa kutoka Bara Uropa.
Aidha, kinakadiriwa kugharimu kima cha Sh100 kukizindua mnamo Januari mwaka ujao, 2022 na kuanza kutengeneza fatalaiza za kipekee.
“Tunatarajia kupokea mashine Oktoba 2021. Baada ya uzinduzi, mkulima yeyote anaweza kututembelea hapa au katika maduka yetu yaliyoko sehemu mbalimbali nchini, na sampuli ya udongo na tutamtengenezea fatalaiza itakayoangazia changamoto za shamba lake,” Mkurugenzi huyo akaambia Taifa Leo wakati wa mahojiano ya kufahamu mpango wake katika makao makuu ya Elgon Kenya yaliyoko Mombasa Road, jijini Nairobi.
“Teknolojia ya mashine tutatakazotumia, ina uwezo kuunda kiwango chochote cha mbolea anachotaka mteja,” Dkt Bimal akaongeza.
Alitoa tangazo la mradi huo mkuu wakati wa hafla ya ukumbusho wa Mwenyekiti wa kampuni hiyo, Bw Rajni Kantaria aliyeaga dunia Agosti 31, 2021.
Marehemu aliombolezwa kama nguzo kuu ya Elgon Kenya, na kumiminiwa sifa kutokana na mchango wake mkuu kusaidia kuboresha sekta ya kilimo nchini.
Wakati akihudumu kama mkurugenzi mkuu na baadaye kupandishwa ngazi kuwa mwenyekiti, Mzee Rajni alizindua miradi mbalimbali kama vile vifaa vya kilimo cha mvungulio (greenhouse) kwa wakulima wa mashamba madogo, upakiaji mpya wa vifaa hivyo na pia vya maua na pembejeo; mbolea, mbegu na dawa za kilimo.
Akitambua jitihada za babake, Dkt Bimal alisema: “Mbali na kusaidia kuboresha sekta ya kilimo, Mzee alikuwa na mchango mkuu katika jamii, ambapo alisaidia wasiojiweza, kuzindua shule na vituo vya afya.”
Ikiwa na matawi katika nchi zote za Ukanda wa Afrika Mashariki, Elgon Kenya Ltd ina vituo 400 vya usambazaji pembejeo nchini na zaidi ya wafanyakazi 1,000.
Bw Rajni pia anakumbukwa kusaidia baadhi ya wafanyakazi wake kukata kiu ya masomo kwa kuwafadhili ili wapate elimu au wajiongezee ujuzi. Alifariki akiwa na umri wa miaka 78.