• Nairobi
  • Last Updated March 29th, 2024 3:04 PM
KAMAU: Mapinduzi yanatoa dalili Afrika imeshindwa kujitawala

KAMAU: Mapinduzi yanatoa dalili Afrika imeshindwa kujitawala

Na WANDERI KAMAU

JE, huenda lilikuwa kosa kwa baadhi ya nchi za Afrika kupewa uhuru na wakoloni?

Pengine hilo ndilo swali linaloweza kuibuka kutokana na msururu wa mapinduzi ya kijeshi ambayo yanaendelea kushuhudiwa katika baadhi ya nchi.

Mwelekeo huo unafanana na kitoto kichanga kilichoruhusiwa kujifanyia maamuzi na mzazi wake bila kufikisha umri wa utu uzima.

Jumapili iliyopita, wanajeshi nchini Guinea walimpindua aliyekuwa rais wa taifa hilo, Alpha Conde, kwa madai ya kuendeleza ufisadi, ukiukaji wa haki za binadamu na kudorora kwa uchumi.

Ijapokuwa katiba ya taifa hilo inawaruhusu marais kuhudumu kwa mihula miwili pekee, Conde alitumia ushawishi wake kubadilisha katiba na kuwania urais kwa muhula wa tatu.

Kwenye matokeo yaliyotolewa baada ya uchaguzi huo uliofanyika Oktoba 2020, Conde alitangazwa kuwa mshindi katika hali tatanishi.

Ushindi wake ulizua maandamano makubwa, raia wakimtaka kung’atuka uongozini kwa kuchukua mamlaka kinyume na taratibu za kisheria zilizopo.

Kwa sasa, taifa hilo lipo kwenye njiapanda, baada ya Muungano wa Afrika (AU) na Jumuiya ya Kiuchumi ya Mataifa ya Afrika Magharibi (ECOWAS) kutishia kuliondoa kama mwanachama wake.

Kando na hayo, nchi za ukanda wa Afrika Magharibi zimetishia kuliwekea vikwazo vya kiuchumi ikiwa wanajeshi hao hawatarejesha uongozi wake kwa raia.

Bila shaka, hizi zimekuwa simulizi za kawaida barani humu.

Kinachoshtua ni kwamba, matukio haya yanatokea katika karne ya 21, wakati baadhi ya jamii zinayaona kama simulizi na hadithi za Alfu Lela Ulela, kwani hazijawahi kuyasikia au yalitokea mara ya mwisho katika miaka ya sitini, sabini au themanini.

Kwa sasa, nchi kama Somalia, Mali, Sudan Kusini, Sudan, Ethiopia kati ya nyingine zinapitia katika vipindi vigumu sana kuhusu mustakabali wazo kisiasa.

Raia hawajui kesho yao itakuwa vipi kutokana na mizozo ya kisiasa inayoendelea.

Kwa mfano, nchini Somalia, imekuwa kama kawaida kwa Rais Mohamed Farmajo kuvutana na viongozi wa vitengo vingine muhimu vya utawala wake.

Nchini Mali, hali ingali tete. Mapinduzi yamekuwa kama jambo la kawaida.

Swali linaibuka: Ni wakati mataifa haya yatawaliwe tena na wakoloni hadi yapevuke kisiasa?

Bila shaka hilo halifai, kwani baadhi ya mataifa ya Ulaya yamelauliwa kwa kuvuruga uthabiti wa kisiasa katika nchi hizo kimakusudi ili kupora raslimali zake asilia.

Ni wakati bara hili lifahamu kuwa linachekwa na maadui wake Waafrika wanapogeukiana wao kwa wao.

[email protected]

You can share this post!

Obiri atawala mbio za kilomita 21 za Great North Run

Serikali kujengea wahasiriwa Laikipia makazi