Na Kenya News Agency
MKURUGENZI wa Shirika la Kitaifa la Huduma kwa Vijana (NYS) Matilda Sakwa amesema kuwa ufisadi ambao umezingira shirika hilo miaka ya nyuma umetokomea na shirika hilo sasa liko katika mkondo mzuri wa uwajibikaji.
Bi Sakwa alisema kuwa NYS haiwezi kurudia makosa hayo ya miaka ya nyuma kwa kuwa yaliipa shirika hilo dhana mbaya machoni pa umma na pia kuathiri bajeti yake huku lengo lao kuu likiwa kuhakikisha umma unaamini katika utendakazi wao.
“Shirika la NYS limepiga hatua na hakuna sakata tena kama miaka ya nyuma. Kuna mambo mazuri na miradi ya kuvutia inayoendelezwa na shirika hili,” akasema Bi Sakwa mjini Ugunja akiwa ameandamana na mbunge wa eneo hilo Opiyo Wandayi.
Aidha, Bi Sakwa aliwataka wazazi wawe huru kuwaruhusu watoto wao wajiunge na NYS akisema serikali itakuwa ikadhamini ili wasomee kozi za kiufundi baada ya kukamilisha mafunzo yao.
Kwa upande wake, Bw Wandayi aliitaka serikali ibuni sera itakayomlazimu kila Mkenya ambaye ana umri wa miaka 18 kupokea mafunzo ya NYS.